Tabora. Jeshi la Polisi mkoani Tabora limewakamata watu 128 kwa makosa mbalimbali, wakiwemo waganga 11 wanaodaiwa kufanya ramli chonganishi bila vibali, huku likisema baadhi ya ramli hizo zimekuwa zikichochea migogoro, mauaji na ukatili katika jamii.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Twaha Lulengelule, amesema hayo Agosti 21, 2026, wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu operesheni zilizofanyika mkoani humo.
Amesema Jeshi la Polisi halitawavumilia watu wanaotumia ramli chonganishi kuchochea migogoro katika familia na jamii, hasa pale zinapotolewa tuhuma zinazoweza kumfanya mtu kuchukua sheria mkononi.
“Hatukubali watu kama hawa ambao wanapiga ramli hizi halafu zinasababisha migogoro kwenye jamii, mauaji na ukatili pia,” amesema.
Kamanda Twaha amesema baadhi ya watu wanaofanya vitendo vya ukatili au matukio mengine ya uhalifu wanapochunguzwa, wakati mwingine hubainika kuwa walipata maelekezo kutoka kwa waganga wanaodaiwa kuwaambia kuwa matatizo yao yamesababishwa na ndugu au watu wengine.
Amesema hali hiyo inaweza kusababisha mtu kuamini tuhuma hizo na kuamua kumdhuru au kumuua mtu anayehisiwa kuwa chanzo cha matatizo yake.
“Mtu anaweza kuambiwa wewe una matatizo muda mrefu, hii ni kwa sababu unalogwa labda na mama yako au bibi yako, sasa mtu anaamua kuchukua sheria mkononi na kuleta madhara,” amesema.
Katika operesheni hizo, Kamanda Twaha amesema polisi pia imewakamata watuhumiwa 14 kwa tuhuma za kukutwa na nyara za wanyamapori.
Amesema watuhumiwa saba walikutwa na meno mawili ya tembo na vipande tisa, huku wengine saba wakikutwa na miguu minane ya swala pamoja na vipande vya ngozi za wanyamapori, ikiwemo ya chui.
Amesema hatua hizo ni sehemu ya operesheni zinazofanywa na Jeshi la Polisi kukabiliana na uhalifu wa aina mbalimbali mkoani humo.
Bangi kilo 512 zakamatwa
Katika taarifa hiyo, Kamanda Twaha amesema katika operesheni iliyofanyika Julai mwaka huu, polisi iliwakamata watuhumiwa 16 waliokuwa na bangi kilo 512 pamoja na kete 1,200.
Amesema katika kipindi hicho pia walikamatwa watu 50 waliokuwa na pombe ya moshi lita 273 pamoja na mtambo mmoja wa kutengeneza pombe hiyo.
Kwa mujibu wa Kamanda Twaha, miongoni mwa watuhumiwa 128 waliokamatwa, 16 wamekwishafikishwa mahakamani na kuhukumiwa vifungo mbalimbali kwa makosa likiwemo mauaji, ubakaji, kupatikana na mali za wizi, kujeruhi, kuharibu mali, kutishia kuua kwa kutumia silaha, shambulio la kudhuru mwili na kutelekeza mtoto.
Amesema Shabani Kilingo amehukumiwa kifungo cha miaka 30 jela kwa kosa la ubakaji, huku Isack Ryangera akihukumiwa kifungo cha nje cha mwaka mmoja kwa kosa la kuua bila kukusudia.
Wakizungumzia operesheni hizo, baadhi ya wakazi wa Tabora wameitaka Serikali kuendelea kuchukua hatua dhidi ya watu wanaohusika na vitendo vya uhalifu na wanaotumia ramli kuchochea migogoro katika jamii.
Hawa Hassani, mkazi wa Tabora, amesema adhabu kali zinahitajika kwa wahalifu, hasa wanaofanya vitendo vya ukatili, ili ziwe fundisho kwa wengine.
“Tumekuwa tukishuhudia watu wanahukumiwa lakini bado hayo makosa yanajirudia. Sasa kuna uwezekano kuwa adhabu zinazotolewa ni rafiki kwao, ndiyo sababu,” amesema.
Mkazi mwingine, Hamisi Kilango, amesema kuwepo kwa waganga wanaofanya shughuli bila vibali kunaweza kuongeza hatari ya watu kufanya vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama wa jamii.
Amesema baadhi ya matukio ya watoto kupotea, kubakwa na kuuawa yanapaswa kuifanya jamii na vyombo vya usalama kuwa makini zaidi.
“Ni miezi michache tu tumeshuhudia watoto wanapotea na wakipatikana ni marehemu, wanabakwa, wanafanyiwa kila aina ya ukatili. Sasa ni wakati sahihi Jeshi la Polisi kuweka mguu chini hasa,” amesema.
Amesema usimamizi wa shughuli zinazohusisha waganga na wanaotoa huduma hizo unapaswa kuimarishwa ili kuzuia matumizi ya ramli yanayoweza kuchochea watu kuchukua sheria mkononi.

Back to Home
11 mbaroni Tabora kwa ramli chonganishi
Mwananchi about 3 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
