Moshi. Geita Gold Mining Limited (GGML) imesema kitendo cha washiriki wake 42 wa kampeni ya GGM HIV Kili Challenge kufika katika kilele cha Mlima Kilimanjaro na kurejea salama kimeipa nguvu kampeni ya kuhamasisha mapambano dhidi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) nchini.
Washiriki hao walipokelewa katika Lango la Mweka na viongozi wa Serikali, wadau na wananchi baada ya kukamilisha safari ya siku kadhaa iliyowapitisha katika njia za Machame, Shira, Lava Tower, Barranco na Barafu kabla ya kufika Uhuru Peak.
Mbali na kundi la wapanda mlima, kampeni ya mwaka huu pia ilihusisha timu ya waendesha baiskeli waliozunguka Mlima Kilimanjaro, wakihamasisha jamii, taasisi na sekta binafsi kuchangia rasilimali kwa ajili ya afua za kupambana na VVU na Ukimwi.
Akizungumza leo Alhamisi, Julai 30, 2026, baada ya kuwapokea, Makamu wa Rais wa AngloGold Ashanti anayesimamia Miradi Endelevu na Mahusiano Barani Afrika, Simon Shayo, amesema mafanikio hayo yanaonesha nguvu ya ushirikiano kati ya sekta binafsi, Serikali na wananchi katika kuendeleza mapambano dhidi ya Ukimwi.
"Tunajivunia kuona washiriki wetu wote wamefanikiwa kufika kileleni na kurejea salama. Huu si ushindi wa kupanda Mlima Kilimanjaro pekee, bali ni ushindi wa dhamira ya pamoja ya kuendelea kupambana na VVU na Ukimwi nchini.
Kila hatua waliyopiga ilikuwa ujumbe wa matumaini kwa maelfu ya Watanzania wanaoishi na VVU pamoja na jamii nzima," amesema.
Amesema kampeni hiyo imeendelea kuwa sehemu ya programu za uwajibikaji kwa jamii za GGML kwa zaidi ya miaka 20, huku fedha zinazokusanywa zikielekezwa katika kusaidia huduma za afya, ununuzi wa vifaa tiba, utoaji wa elimu kwa jamii, kusaidia vituo vya malezi na kutekeleza afua mbalimbali za kupunguza maambukizi mapya ya VVU.
Shayo amesema ushirikiano huo umeendelea kuunga mkono juhudi za Serikali za kufikia malengo ya Sifuri Tatu ifikapo mwaka 2030, yanayojumuisha kutokomeza maambukizi mapya ya VVU, vifo vinavyotokana na Ukimwi na unyanyapaa dhidi ya watu wanaoishi na VVU.
Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (TACAIDS), Nyangasi Laizer, amesema kampeni hiyo imeendelea kuwa mfano wa namna sekta binafsi inavyoweza kushirikiana na Serikali katika kukabiliana na changamoto za afya ya umma.
Amesema umuhimu wa ushirikiano huo unaongezeka wakati ambapo misaada ya kifedha kutoka nje kwa ajili ya mapambano dhidi ya Ukimwi inaendelea kupungua, hivyo kuifanya Tanzania kuimarisha matumizi ya rasilimali za ndani kufanikisha afua mbalimbali.
"GGM HIV Kili Challenge imeendelea kuwa kampeni yenye matokeo makubwa. Mbali na kuchangisha fedha, imekuwa jukwaa la kutoa elimu, kuhamasisha upimaji wa hiari wa VVU, uchangiaji wa damu salama na kupunguza unyanyapaa dhidi ya watu wanaoishi na VVU," amesema.
Nahodha msaidizi wa kundi la wapanda mlima, Chitegetse Rushatsi, amesema changamoto za safari hiyo hazikuwavunja moyo washiriki, bali zilizidi kuwapa nguvu ya kutimiza lengo la kuhamasisha jamii kushiriki katika mapambano dhidi ya VVU na Ukimwi.
Mbali na upandaji wa Mlima Kilimanjaro, kampeni ya mwaka huu ilijumuisha upimaji wa hiari wa VVU, uchangiaji wa damu salama, upandaji wa miti kwa ajili ya uhifadhi wa mazingira na shughuli mbalimbali za uelimishaji wa jamii.

Back to Home
42 wa GGM wafika kilele cha Mlima Kilimanjaro
Mwananchi about 4 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
