Mtwara. Bodi ya Korosho Tanzania (CBT) imewaonya wabanguaji wanaokiuka taratibu za ununuzi wa korosho katika soko la awali, ikisema itachukua hatua kwa kuwa vitendo hivyo vinawaathiri wakulima na kuvuruga mfumo wa biashara ya zao hilo.
Katika kushughulikia tatizo hilo, CBT imeinyima kampuni moja kibali cha kununua korosho baada ya kudaiwa kuchukua, kubangua na kuuza korosho za wakulima bila kuwalipa.
Hatua hiyo inalenga kulinda wakulima na kuhakikisha utaratibu wa soko la awali unafuatwa.
Akizungumza katika mahojiano maalumu na Mwananchi, Mkurugenzi Mkuu wa CBT, Francis Alfred amesema baadhi ya kampuni zimekuwa zikichukua korosho za wakulima bila kufanya malipo kwa wakati, kinyume na utaratibu unaowataka wanunuzi kulipa fedha za korosho pamoja na tozo husika.
Alfred amesema baadhi ya wabanguaji wamekuwa wakitumia ushawishi kwa viongozi wa Amcos ili kupata korosho kwa makubaliano yasiyo rasmi, hali inayosababisha wakulima kucheleweshewa malipo.
“Baadhi ya kampuni hazifuati utaratibu, wanakwenda kuchukua korosho za wakulima, halafu wanawaambia watalipa baadaye. Wakati utaratibu wa soko la awali unasema hutakiwi kuchukua korosho za wakulima bila kulipa,” amesema.
Amesema CBT imechukua hatua dhidi ya kampuni moja (hajaitaja jina), inayodaiwa kuchukua korosho za wakulima, kuzibangua na kuziuza bila kuwalipa, kwa kuizuia kufanya shughuli zake katika vituo vya ununuzi.
Kwa mujibu wa Alfred, CBT haijabadilisha utaratibu wa soko la awali, bali inasimamia utekelezaji wa masharti yaliyowekwa na Serikali ili kuhakikisha biashara inafanyika kwa uwazi na masilahi ya mkulima yanalindwa.
Aidha, amesema CBT imeanza kufuatilia matumizi ya mawakala katika ununuzi wa korosho, ikisisitiza kuwa mawakala hao wanapaswa kusajiliwa na kutambulika rasmi.
“Kwa wale ambao wangependa kutumia mawakala kununua korosho, tunataka mawakala hao wasajiliwe na Bodi ya Korosho Tanzania. Hatutaruhusu mbanguaji atumie wakala ambaye hajasajiliwa,” amesema.
Amesema uwepo wa mawakala wasiotambulika unaweza kufanya iwe vigumu kutofautisha kati ya mawakala halali, kangomba na wanunuzi wengine, hivyo kusababisha vurugu katika vituo vya ununuzi.
Katika hatua nyingine, CBT imepanga kuimarisha udhibiti wa mizigo ya korosho kabla haijatoka katika wilaya husika, kwa kuwaweka maofisa katika vituo maalumu vya uhakiki.
Kwa mujibu wa Alfred, maofisa hao watathibitisha kiasi cha korosho na uhalali wa vibali kabla ya mizigo kusafirishwa, hatua inayolenga kudhibiti ukwepaji wa tozo na kuhakikisha mizigo inayosafirishwa inaendana na vibali vilivyotolewa.
Wakati CBT ikitoa onyo hilo, Chama cha Wabanguaji Korosho nchini (TAPC), kimeiomba Serikali kuweka mikakati zaidi ya kukuza sekta ya ubanguaji, ikisema bado inakabiliwa na changamoto zinazokwamisha ukuaji wake.
Mwenyekiti wa TAPC, Sosthenes Mayoma amesema sekta hiyo inalenga kuongeza ajira kutoka 14,000 zilizopo sasa hadi 50,000 ifikapo mwaka 2030.
Amesema ili kufikia lengo hilo, Serikali inapaswa kuwawezesha wabanguaji kwa kuondoa vikwazo vinavyokabili sekta hiyo na kuongeza uwekezaji katika ubanguaji wa korosho nchini.
Farida Juma, mbanguaji kutoka Newala, amesema kuwawezesha wabanguaji wadogo kwa teknolojia na vifaa vya kisasa kutasaidia kuongeza uzalishaji na ushindani.
Amesema ukosefu wa teknolojia na vifaa vya kisasa ni miongoni mwa changamoto zinazowakabili, akisisitiza kuwa mafunzo na nyenzo bora vinaweza kuongeza ufanisi wa sekta hiyo.
Inaelezwa kuwa sekta ya ubanguaji ina uwezo wa kutoa ajira zaidi ya 100,000, hususan kwa wanawake na vijana, endapo uwekezaji na mazingira rafiki ya biashara yataimarishwa.

Back to Home
Bodi ya Korosho ‘kuwashughulikia’ wabanguaji wanaokiuka utaratibu
Mwananchi about 2 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
