Njombe. Wafanyabiashara wa pembejeo za kilimo wilayani Njombe wameonywa dhidi ya kupandisha bei ya mbolea kwa kisingizio cha kuongezeka kwa gharama za mafuta, huku Serikali ikisisitiza kuwa tayari imetoa ruzuku ili kuwapa nafuu wakulima.
Onyo hilo limetolewa leo Jumanne Mei 19, 2026, na Mkuu wa Wilaya ya Njombe, Juma Sweda wakati wa ufunguzi wa Maonyesho ya Mbegu na uzinduzi wa mbegu mpya ya mahindi ulioandaliwa na Kampuni ya Kibo Seed katika Kata ya Majengo, mjini Makambako.
Sweda amesema Serikali tayari imechangia gharama za mbolea kupitia ruzuku, hivyo hakuna sababu kwa wafanyabiashara kuongeza bei na kuwaumiza wakulima.
Amesema wafanyabiashara watakaobainika kuuza mbolea nje ya bei elekezi ya ruzuku watachukuliwa hatua za kisheria, huku akiwaomba wakulima kutoa taarifa kwa mamlaka husika pale wanapokutana na ukiukwaji huo.
“Marufuku kupandisha bei ya mbolea kwa sababu Serikali imelipia sehemu ya gharama hizo. Wapo wanaotaka kutumia changamoto za mafuta kama sababu ya kuongeza bei, hilo halitakubalika,” amesema Sweda.
Katika hatua nyingine, amewataka wadau wa kilimo kuhakikisha uzalishaji na usambazaji wa mbegu bora unasimamiwa ipasavyo ili kudhibiti mbegu feki zinazowaingiza hasara wakulima.
Mkuu wa Idara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi wa Halmashauri ya Mji wa Makambako, Beatrice Tarimo amesema wakulima wanapaswa kupima afya ya udongo mara kwa mara badala ya kutegemea mbegu bora pekee kuongeza uzalishaji.
Amesema kupungua kwa rutuba ya udongo ni moja ya sababu zinazochangia mavuno hafifu kwa wakulima wengi.
“Udongo unaolimwa kwa miaka mingi hubadilika kiwango cha rutuba, hivyo ni muhimu kupima afya ya udongo ili kujua mahitaji yake kabla ya msimu wa kilimo,” amesema Tarimo.
Ameeleza kuwa Serikali imetoa huduma ya upimaji wa afya ya udongo bila malipo kupitia maofisa ugani waliopo katika maeneo mbalimbali.
Naye Ofisa Masoko wa Kampuni ya Kibo Seed, Ombeni Kileo, amesema maonyesho hayo yamelenga kuwawezesha wakulima kutambua mbegu bora pamoja na kusaidia kudhibiti usambazaji wa mbegu bandia sokoni.
“Tunataka mkulima apate mbegu bora na zinazomletea tija, huku tukisaidia kupunguza changamoto ya mbegu feki zinazowaathiri wakulima wengi,” amesema Kileo.
Baadhi ya wakulima kutoka mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, ikiwamo Njombe, Iringa, Mbeya na Ruvuma, wameiomba Serikali kuongeza udhibiti dhidi ya wauzaji wa mbegu bandia wanaosababisha hasara kwa wakulima.
Wamesema changamoto hiyo imekuwa ikiathiri uzalishaji wao na kuongeza gharama za kilimo licha ya jitihada zinazofanywa na Serikali kuboresha sekta hiyo.