TRENDING
‘Dunia ifanye hivi kulinda afya za watoto zama hizi za dijitali’
Back to Home

‘Dunia ifanye hivi kulinda afya za watoto zama hizi za dijitali’

Mwananchi about 5 hours 5 mins read
Dar es Salaam. Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron na Mkurugenzi wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Tedros Ghebreyesus, wametoa wito kwa Serikali kuharakisha hatua za kuwalinda watoto dhidi ya athari za mazingira ya kidijitali. Viongozi hao wamesema teknolojia imekuwa na mchango mkubwa katika afya na maendeleo ya watoto, lakini pia imeongeza hatari zinazohitaji udhibiti wa haraka. Katika makala yao iliyochapishwa hivi karibuni, viongozi hao wanasema matumizi ya mitandao ya kijamii, michezo ya mtandaoni na mifumo ya akili unde (AI) yamebadili namna watoto wanavyojifunza, kucheza na kuwasiliana, hivyo kufanya mazingira ya kidijitali kuwa sehemu muhimu inayochangia afya zao. Pamoja na manufaa ya teknolojia katika elimu, mawasiliano na upatikanaji wa huduma za afya, hasa kwa watoto wanaoishi maeneo ya mbali au yanayokumbwa na migogoro, bado manufaa hayo hayawezi kupatikana bila kuwepo kwa mifumo madhubuti ya ulinzi. Kwa mujibu wa viongozi hao, Serikali mbalimbali zimeanza kuchukua hatua za kudhibiti matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watoto. Mataifa kama Australia, France, Indonesia, Spain, Ireland, Uingereza na Canada yameanzisha au yanatekeleza sheria zinazoweka umri wa chini wa kutumia mitandao ya kijamii pamoja na kuongeza mifumo ya uthibitishaji wa umri na usalama kwa watoto. Wanasema hatua hizo zinaonyesha kuwepo kwa makubaliano ya kimataifa kwamba mazingira ya kidijitali yanahitaji kusimamiwa kwa karibu kupitia sheria, uwajibikaji wa kampuni za teknolojia na ubunifu unaoweka mbele usalama wa watoto. Katika makala hiyo, Macron na Tedros wanaeleza kuwa ushahidi uliopo unaonyesha matumizi ya kupita kiasi ya teknolojia yanahusishwa na ongezeko la matatizo ya afya ya akili ikiwemo msongo wa mawazo, wasiwasi, kukosa usingizi, tabia za ukatili na hata hatari ya kujiua kwa baadhi ya vijana walio katika mazingira hatarishi. Pia wanaonya kuwa algoriti zinazotumika kwenye majukwaa ya kidijitali mara nyingi husambaza taarifa zinazolenga kuvutia watumiaji badala ya kuhakikisha usahihi wake, jambo linaloweza kuchochea upotoshaji wa taarifa za afya. Aidha, ukusanyaji wa taarifa binafsi za watoto kwa ajili ya matangazo yanayolengwa unazua hofu kuhusu faragha na ustawi wao. Mbali na hilo, viongozi hao wanasema watoto wanaendelea kukumbwa na ongezeko la ukatili wa kingono mtandaoni, usambazaji wa picha za unyanyasaji zinazotengenezwa kwa kutumia AI pamoja na maudhui ya udhalilishaji yanayotumia teknolojia ya 'deepfake', hali inayoweza kuacha athari za muda mrefu kwa afya ya akili na usalama wao. Wanasema changamoto hizo zinaongezwa na mifumo ya kibiashara ya baadhi ya kampuni za teknolojia ambazo hubuni majukwaa yanayolenga kuwafanya watumiaji wabaki mtandaoni kwa muda mrefu bila kuweka ulinzi wa kutosha dhidi ya maudhui hatarishi. Kwa upande wa AI generative, Macron na Tedros wanasema teknolojia hiyo inaweza kuleta mapinduzi katika elimu, huduma za afya na upatikanaji wa taarifa ikiwa itatumika kwa uwajibikaji. Hata hivyo, wanaonya kuwa athari zake za muda mrefu katika maendeleo ya kihisia, uhusiano wa kijamii na uwezo wa watoto kujidhibiti bado hazijafahamika kikamilifu. Kutokana na hali hiyo, wanasisitiza umuhimu wa kuweka uwiano kati ya matumizi ya teknolojia na maisha ya kawaida, huku wakitaka kuwepo kwa utafiti huru unaoendana na kasi ya maendeleo ya teknolojia ili kusaidia utungaji wa sera na sheria. Pia wanatoa wito kwa wazazi, walimu, jamii, sekta binafsi na serikali kushirikiana katika kujenga mazingira salama ya kidijitali, wakiamini kuwa watoto na vijana wenyewe wanapaswa kushirikishwa katika kubuni sera na kanuni zitakazolinda maslahi yao. "Watoto wetu si maabara ya majaribio, si soko la bidhaa wala bidhaa yenyewe. Maamuzi tunayofanya leo kuhusu mazingira ya kidijitali yataathiri vizazi vijavyo.” Jinsi ya kuwalinda Katika makala hiyo, Macron na Tedros wamependekeza hatua kadhaa za kuwalinda watoto katika mazingira ya kidijitali. Hatua hizo ni kuweka sheria za umri wa kutumia mitandao ya kijamii. Mosi, Mataifa yaweke kikomo cha umri wa kufungua akaunti za mitandao ya kijamii, hasa kwa watoto walio chini ya miaka 16. Kutumika mifumo ya kuthibitisha umri, kubuni majukwaa yanayozingatia usalama wa watoto, Kampuni za teknolojia zijenge mifumo inayowalinda watoto tangu hatua ya kubuni programu. Kupunguza uwezekano wa watoto kuona maudhui hatarishi au kuwasiliana na watu wasiowafahamu, kuongeza uwazi na uwajibikaji wa kampuni za teknolojia. Kampuni ziwe wazi kuhusu namna algoriti zinavyofanya kazi, ziwajibike kwa madhara yanayosababishwa na majukwaa yao, hasa kwa watoto. Kudhibiti maudhui hatarishi, kupunguza au kuondoa maudhui ya ukatili, ngono, ubaguzi na maudhui mengine yenye madhara. Kudhibiti taarifa potofu, hasa zinazohusu afya. Kulinda faragha za watoto, kupunguza ukusanyaji wa taarifa binafsi za watoto. Kudhibiti matangazo yanayolenga watoto kwa kutumia taarifa zao binafsi. Kuweka uwiano wa matumizi ya teknolojia, kuhamasisha watoto wasitumie muda mwingi mtandaoni, kukuza michezo ya nje, mazoezi ya mwili na mahusiano ya ana kwa ana ili kupunguza upweke na matatizo ya afya ya akili. Kuwekeza katika tafiti, kufanya tafiti za muda mrefu kuhusu athari za mitandao ya kijamii na AI kwa afya ya watoto ili sera ziendane na ushahidi wa kisayansi. Kwa ujumla, hoja kuu ya Macron na Tedros ni kwamba ulinzi wa watoto mtandaoni haupaswi kubebwa na wazazi pekee, bali unahitaji sheria madhubuti, uwajibikaji wa kampuni za teknolojia na ushirikiano wa jamii nzima ili kuhakikisha teknolojia inawanufaisha watoto bila kuhatarisha afya na maendeleo yao.

This article was sourced from an external publication.

Share this article

Comments (0)

Want to join the discussion?

Sign in to post comments and engage with the community.

Be the first to comment!

OneClick Africa Logo

Africa's premier digital hub for impactful news, entertainment, and business insights.

© 2026 OneClick Africa. All rights reserved.