TRENDING
Hillary Clinton ataka mfumo wa kumpata Rais Marekani ubadilishwe
Back to Home

Hillary Clinton ataka mfumo wa kumpata Rais Marekani ubadilishwe

Mwananchi about 2 hours 5 mins read
Dar es Salaam. Kauli ya sasa ya aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha Democratic nchini Marekani, Hillary Clinton, akitaka kufutwa mfumo wa kumpata Rais kupitia kura za wajumbe maalumu (Electoral College), imefungua upya vidonda vya kisiasa na kuibua mjadala wa miaka mingi kuhusu uhalali wake katika uchaguzi mkuu wa nchi hiyo. Clinton, ambaye alikumbana na rungu la mfumo huo katika uchaguzi mkuu wa mwaka 2016, amenukuliwa akisema: “Huu mfumo unapaswa kuondoka. Hatupaswi kung'ang'ania kitu kilichopitwa na wakati, ambacho kiliundwa kwa ajili ya majimbo yaliyokuwa yakimiliki watumwa. Hebu tuutazame upya kwa ajili ya karne ya 21.” Kauli hiyo imetafsiriwa na baadhi ya wachambuzi wa masuala ya kisiasa kama mwendelezo wa shinikizo kutoka kwa wanasiasa wa Chama cha Democratic wanaotaka kura za wananchi (popular vote) ndizo ziamue nani anakuwa Rais wa Marekani. Maana, asili ya Electoral College Tofauti na nchi nyingi duniani ambako rais hupatikana kwa kuhesabu kura za wananchi moja kwa moja (popular vote), Marekani hutumia mfumo wa kipekee. Wananchi wanapopiga kura, hawamchagui Rais moja kwa moja. Badala yake, wanachagua wajumbe maalumu (electors), ambao ndio huunda Electoral College na kupiga kura ya mwisho ya kumchagua Rais. Idadi ya wajumbe ni 538 Ili mgombea atangazwe kuwa Rais wa Marekani, anahitaji kupata angalau kura 270 kati ya kura 538 za wajumbe wanaotokana na mgawanyo wa majimbo. Kila jimbo linapewa idadi fulani ya wajumbe kulingana na idadi ya wabunge wake katika Bunge la Congress (linalojumuisha Seneti na Baraza la Wawakilishi). Kwa mfano, majimbo makubwa kama California yana wajumbe wengi, 54, wakati majimbo madogo kama Wyoming yana wajumbe watatu. Kanuni ya "mshindi anachukua vyote" (winner-take-all) inatumika katika majimbo mengi isipokuwa Maine na Nebraska. Mgombea anayeshinda kura nyingi zaidi za wananchi katika majimbo hayo, hata kama ni kwa tofauti ya kura moja tu, hupata kura zote za wajumbe (electoral votes) wa jimbo hilo. Kwa mfano, kama mgombea A akipata asilimia 51 ya kura za wananchi wa Florida na mgombea B akapata asilimia 49, kura zote 30 za wajumbe wa Florida huenda kwa mgombea A. Hii ina maana kuwa kura za asilimia 49 ya wananchi waliomchagua mgombea B hazina nguvu tena katika matokeo ya jimbo hilo. Mtego wa kihistoria Tofauti kati ya ushindi wa kura za wananchi na ushindi wa kura za Electoral College imekuwa mtego kwa wagombea kadhaa, akiwamo Hillary Clinton. Mgombea anaweza kushinda kura nyingi za wananchi kitaifa, lakini bado akashindwa urais kwa kukosa kura za kutosha za Electoral College. Katika historia ya Marekani, jambo hili limetokea mara tano. Kwa mfano, mwaka 2016 Hillary Clinton alipata kura za wananchi milioni 2.9 zaidi ya Donald Trump. Hata hivyo, Trump alishinda majimbo muhimu (swing states) kama Pennsylvania, Michigan na Wisconsin kwa tofauti ndogo ya kura, jambo lililompa kura 304 za wajumbe dhidi ya 227 za Clinton, na hivyo kuwa Rais. Mwaka 2000, Al Gore (Democrat) aliongoza kwa kura za wananchi kitaifa, lakini George W. Bush (Republican) akatwaa urais baada ya kushinda kura za Electoral College kufuatia mzozo mkubwa wa kura Florida. Sababu ya Electoral College Mfumo huu ulianzishwa mwaka 1787 wakati wa kuandikwa kwa Katiba ya Marekani. Sababu kuu ya kwanza ilikuwa hofu ya majimbo yenye watu wachache kwamba kama kura za wananchi zingetumika moja kwa moja, majimbo makubwa yenye idadi kubwa ya watu, kama New York na Virginia wakati huo, yangekuwa yanaamua rais katika kila uchaguzi, huku majimbo madogo yakikosa sauti. Sababu ya pili ilikuwa suala la utumwa, na hapa ndipo hoja ya Clinton inapotegemea. Wakati huo, majimbo ya Kusini yalikuwa na idadi kubwa ya watumwa ambao hawakuwa na haki ya kupiga kura. Kama kura za wananchi zingetumika moja kwa moja, majimbo ya Kaskazini, ambako watumwa walikuwa wachache, yangekuwa na nguvu zaidi. Kupitia maridhiano ya kikatiba (Three-Fifths Compromise), watumwa walihesabiwa kama tatu ya watano (3/5) ya mtu kwa madhumuni ya kuhesabu uwakilishi wa majimbo hayo katika Congress. Hali hiyo iliongeza idadi ya wajumbe wa Electoral College kwa majimbo ya Kusini bila kuwaruhusu watumwa hao kupiga kura. Hoja ya Clinton, wenzake Clinton na wanaotaka mfumo huo ufutwe wanajenga hoja kwamba unavunja kanuni ya "mtu mmoja, kura moja, thamani sawa." Wanasema kura ya mkazi wa jimbo dogo kama Wyoming ina uzito mkubwa zaidi kihesabu kuliko kura ya mkazi wa California. Pia, wanaopinga mfumo huo wanasema huwafanya wagombea kupuuza majimbo mengi. Badala yake, hutumia mabilioni ya dola kufanya kampeni katika majimbo machache ya swing states au battleground states kama Pennsylvania na Georgia, kwa sababu ndiyo yanayoamua ushindi. Hoja za wanaotaka Electoral College iendelee Wanaounga mkono mfumo huo wanasema unawalazimisha wagombea urais kujenga ushirikiano wa kitaifa badala ya kujikita katika miji mikubwa yenye watu wengi pekee. Pia, wanasema mfumo huo unahakikisha kila jimbo lina mamlaka ya kusimamia na kuendesha uchaguzi wake, jambo linalofanya iwe vigumu kwa mamlaka ya kitaifa kuathiri matokeo ya uchaguzi wa nchi nzima kwa wakati mmoja. Uwezekano wa mfumo kufutwa Kisheria, kufuta kabisa Electoral College kunahitaji mabadiliko ya Katiba ya Marekani. Jambo hili ni gumu kwa sababu linahitaji uungwaji mkono wa theluthi mbili ya Bunge la Congress na uidhinishaji wa robo tatu ya majimbo yote 50. Majimbo madogo na Chama cha Republican hawawezi kukubali mabadiliko hayo kwa urahisi kwa sababu mfumo wa sasa unawanufaisha kisiasa. Hata hivyo, kuna harakati mbadala inayoitwa National Popular Vote Interstate Compact. Haya ni makubaliano ambapo majimbo yanaapa kisheria kwamba yatatoa kura zao zote za Electoral College kwa mgombea atakayeshinda kura nyingi za wananchi kitaifa. Makubaliano hayo yataanza kutumika mara tu majimbo yenye jumla ya kura 270 za Electoral College yatakapoyaridhia. Hadi katikati ya mwaka 2026, majimbo 19 yalikuwa yameshasaini makubaliano hayo.

This article was sourced from an external publication.

Share this article

Comments (0)

Want to join the discussion?

Sign in to post comments and engage with the community.

Be the first to comment!

Senegal

View All
AD

Traditional Affairs

View All

DR Congo

View All

Somalia

View All
AD
OneClick Africa Logo

Africa's premier digital hub for impactful news, entertainment, and business insights.

© 2026 OneClick Africa. All rights reserved.