Dar es Salaam. Mahakama Kuu Masjala Ndogo Dar es Salaam imemkuta na kesi ya kujibu Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu katika kesi ya uhaini inayomkabili.
Uamuzi huo umetolewa leo Ijumaa, Agosti 21, 2026 na kusomwa na kiongozi wa jopo la majaji watatu wanaosikiliza kesi hiyo, Dunstan Ndunguru kwa niaba ya wenzake Jaji James Karayemaha na Ferdinand Kiwonde.
Jaji Ndunguru katika uamuzi huo amesema baada ya kupitia na kuzingatia ushahidi wa upande wa mashtaka na hoja za mshtakiwa wameona ana kesi ya kujibu.
Lissu anashtakiwa kwa kosa la uhaini kinyume na kifungu cha 39(2) (d) cha Sheria ya Kanuni ya Adhabu iliyorekebishwa mwaka 2023.
Kosa hilo linatokana na maneno aliyoyatamka katika mkutano wake, ofisi za Makao Makuu ya Chadema, Aprili 3, 2025, jijini Dar es Salaam, kuhusiana na msimamo wa kutokushiriki Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025 na nia ya kuuzuia uchaguzi huo.
Katika shtaka hilo anadaiwa kuwa siku hiyo akiwa raia wa Tanzania, kwa nia ya uchochezi alishawishi umma kuzuia kufanyika kwa Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, kwa kutamka na kuandika maneno ya kumshinikiza kiongozi Mkuu wa Serikali ya Tanzania.
Katika maneno hayo yanayodaiwa kuwa ya uhaini, Lissu alitamka kuwa: "Wakisema msimamo huu unaashiria uasi, ni kweli..., kwa sababu tunasema tutazuia uchaguzi, tutahamasisha uasi, hivyo ndivyo namna ya kupata mabadiliko..., kwa hiyo tunaenda kikinukisha..., sana sana huu uchaguzi tutaenda kuuvuruga kwelikweli..., tunaenda kukinukisha vibaya sana..."
Akisoma uamuzi huo, Jaji Ndunguru amesema kuwa katika hatua hii, kinachoangaliwa na mahakama ni iwapo ushahidi uliowasilishwa ukiachwa hivyo mshtakiwa anaweza kutiwa hatiani na kwamba mahakama haitakiwi kuingia kwa undani kuchambua ushahidi huo na kuaminika kwake.
Katika kufikia hitimisho la uamuzi wake mahakama imezingatia viini vitatu vya kosa la uhaini kama vimethibitishwa na upande wa mashtaka.
Viini hivyo vitatu mshtakiwa ana utii kwa Jamhuri.
Hivyo Jaji Ndunguru amesema kuwa kwa kuzingatia kuwa mshtakiwa alikiri ni raia wa Tanzania na shahidi wa 17 ambaye alikuwepo katika mkutano huo alisema kuwa mshtakiwa alitamka maneno hayo mbele ya viongozi wengine wa chama hicho.
Amesema ushahidi wote unamuunganisha mshtakiwa na yale yaliyoko katika hati ya mashtaka.
"Hivyo basi mahakama hii inaona kwamba mahtakiwa ana haki ya kujitetea dhidi ya ushahidi huu ulioletwa na upande wa mashtaka," amesema Jaji Ndunguru.

Back to Home
Lissu akutwa na kesi ya kujibu, Mahakama Kuu yaamua
Mwananchi about 2 hours 2 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
