Mbeya. Wananchi wa Wilaya ya Kyela mkoani Mbeya wametakiwa kuwa mabalozi wa kulinda mazingira na kuhifadhi vyanzo vya maji, kufuatia kupokea majiko safi ya kupikia yanayolenga kupunguza matumizi ya kuni na mkaa pamoja na kuboresha afya za watumiaji.
Hatua hiyo imekuja sambamba na mpango wa kampuni ya Envotec kusambaza majiko banifu zaidi ya 9,000 mkoani Mbeya, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kupunguza gharama za nishati, kulinda mazingira na kuboresha maisha ya wananchi wa kipato cha chini.
Akizungumza Mei 15 wakati wa uzinduzi wa ugawaji wa majiko 513 kwa wakazi wa Kyela, Mkuu wa Wilaya hiyo, Josephin Manase, amewataka wanufaika kuhakikisha wanayatunza majiko hayo na kuyatumia ipasavyo badala ya kuyapuuza au kuyatelekeza.
Amesema Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imewekeza fedha nyingi katika kuhakikisha wananchi wanapata nishati safi, hivyo ni wajibu wa kila mwananchi kuhakikisha anachangia kulinda uwekezaji huo.
“Haya ni majiko safi na ya kisasa. Tukiyatumia vyema tutaondokana na uharibifu wa mazingira. Tuache matumizi ya kuni kwa ajili ya kulinda afya zetu,” amesema Manase.
Ameongeza kuwa kila mwananchi anapaswa kuwa sehemu ya juhudi za uhifadhi wa mazingira kwa kulinda miti na vyanzo vya maji ili kupunguza athari za ukame na ongezeko la joto katika eneo hilo.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kyela, Florah Luhala, ameishukuru kampuni ya Envotec kwa kuleta mradi huo, lakini akibainisha kuwa bado mahitaji ya majiko safi ni makubwa ukilinganisha na idadi iliyotolewa.
“Tunaishukuru Serikali na wadau, lakini majiko 513 hayatoshi. Tunaomba idadi iongezwe ili kuwafikia wananchi wengi zaidi,” amesema Luhala.
Mkurugenzi wa Envotec, Sylivester Mwambije, amesema lengo la kampuni hiyo ni kuwafikia zaidi ya wananchi 9,000 mkoani Mbeya, huku akisisitiza kuwa mradi huo unalenga kuboresha afya na kulinda mazingira kwa wakati mmoja.
Amesema matumizi ya nishati isiyo salama bado ni changamoto kubwa kiafya, hasa kwa wanawake na watoto wanaoathirika zaidi na moshi wa kuni jikoni.
“Majiko haya yamebuniwa kwa usalama na ubora ili kupunguza matumizi ya kuni na kulinda afya za watumiaji,” amesema Mwambije.
Baadhi ya wanufaika wa majiko hayo wameeleza kufurahishwa na mradi huo wakisema utawasaidia kupunguza gharama za maisha pamoja na kuboresha afya.
Yahaya Mwangane amesema majiko hayo yatapunguza matumizi ya kuni na kuwa msaada mkubwa katika kipindi hiki cha kupanda kwa gharama za maisha.
“Tunaomba Serikali iangalie uwezekano wa kuongeza ruzuku ili wananchi wengi zaidi wanufaike,” amesema.
Naye Tegemeo France amesema majiko hayo ni muhimu hasa kwa wanawake wanaotumia muda mwingi jikoni, akisema yatapunguza gharama na madhara ya kiafya yanayosababishwa na moshi.
“Kwa sasa jiko tunalipia Sh 7600 badala ya Sh 50,580 kufuatia ruzuku ya serikali, hii ni fursa kubwa kwetu wananchi haswa wa kipato cha chini na tunaomba huduma iwafikie wengi kwakuwa gharama za maisha ni ghali” amesema Tegemeo.