Unguja. Rais, Samia Suluhu Hassan amezitaka mamlaka za mipango miji Zanzibar kutenga maeneo maalumu kwa ajili ya viwanja vya michezo na burudani za watoto na kuhakikisha hayavamiwi kwa matumizi mengine.
Ametoa agizo hilo leo Jumatano, Agosti 12, 2026, wakati akizindua kiwanja cha watoto Kizimkazi, Kusini Unguja, ikiwa ni sehemu ya shamrashamra za Tamasha la Kizimkazi 2026.
Amesema mara nyingi maeneo yanayotengwa kwa ajili ya watoto huishia kutumika kwa shughuli nyingine, hali inayowanyima sehemu salama za kucheza na kujifunza kupitia michezo.
“Mara nyingi maeneo yanayotengwa kwa ajili ya watoto huishia kutumika kwa shughuli nyingine baada ya muda mfupi, hali inayowanyima watoto sehemu salama za kuchezea na kujifunza kupitia michezo,” amesema Rais huyo.
Hivyo, amezitaka wizara na mamlaka husika kusimamia maeneo hayo ipasavyo, huku akiwakaribisha wawekezaji wa sekta binafsi kushiriki katika ujenzi na uendelezaji wa miundombinu ya watoto.
Amesema viwanja hivyo si sehemu ya burudani pekee, bali ni mazingira muhimu katika malezi na makuzi ya watoto kwa kuwa michezo huwajengea nidhamu, ubunifu, heshima, ushirikiano na kujiamini, pamoja na kuchangia afya ya mwili na akili.
Hata hivyo, ameitaka mamlaka inayosimamia viwanja hivyo kuhakikisha vinatumika kwa kuzingatia maadili ya watoto wenye umri wa miaka mitatu hadi 15.
Amesisitiza matumizi ya teknolojia, ikiwamo muziki, filamu na michezo ya kielektroniki, yaendane na umri wa watoto na kuzingatia mila, desturi na maadili ya jamii.
Rais Samia pia amekemea uwezekano wa kuonyeshwa picha au maudhui yasiyofaa katika maeneo hayo, akisema viwanja vya watoto vinapaswa kuwa sehemu salama ya malezi, burudani na kujifunza.
Katika suala la usalama, amepongeza matumizi ya mchanga katika maeneo ya bembea badala ya sakafu ngumu, akisema hatua hiyo inaweza kupunguza madhara kwa watoto wanapoanguka wakati wa kucheza.
Amesema uwepo wa viwanja hivyo umeanza kuchochea utalii wa ndani, huku wananchi kutoka maeneo mbalimbali ya Unguja wakisafiri kwenda Kizimkazi kuvitembelea.
Kutokana na hali hiyo, amewakaribisha wawekezaji kuongeza huduma zinazowahusu watoto, ikiwemo maduka ya vichezea na maeneo mengine ya burudani na kujifunzia.
Pia, amekabidhi rasmi viwanja hivyo kwa uongozi wa mkoa na wilaya huku akisisitiza mapato yatakayopatikana yatunzwe na kutumika katika matengenezo ili viwanja hivyo vidumu.
Aidha, amewataka wazazi na walezi kuwalea watoto katika misingi ya imani, maadili na upendo, akisema urithi mkubwa zaidi si mali pekee, bali ni taifa salama na lenye amani.
Naye Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Anna Atanas Paul amesema watoto wa vijijini wanastahili mazingira bora ya kucheza, kujifunza na kukuza vipaji.
Amesema kuna umuhimu wa kuwa na vituo kama hivyo katika mikoa yote ya Zanzibar ili watoto wapate fursa sawa ya kukua kimwili, kiakili na kijamii.
Kwa mujibu wa Anna, wizara imeanza kuwafikia watoto wa vijijini kupitia uanzishwaji wa vituo vya kulelea watoto mchana vinavyolenga kutoa huduma za malezi na masomo tangu umri mdogo, ikiwemo miaka miwili.
“Serikali inalenga kuhakikisha tofauti ya fursa kati ya watoto wa mijini na vijijini inapungua, huku kila mtoto akipewa nafasi ya kuanza safari yake ya maisha katika mazingira bora,” amesema.
Mkuu wa Mkoa wa Kusini Unguja, Hamida Mussa Khamis, amesema mkoa huo umeendelea kuongeza fursa kwa watoto kupata maeneo salama ya kucheza na kujenga afya.
Amesema viwanja hivyo vimeandaliwa kwa ajili ya watoto wenye umri wa mwaka mmoja hadi 15, huku ongezeko la watoto na maendeleo ya mkoa huo likiongeza umuhimu wa kujenga viwanja zaidi ili kuwaepusha kucheza katika mazingira yasiyo salama.

Back to Home
Rais Samia atoa tahadhari kwa viwanja vya watoto, aonya wavamizi
Mwananchi about 3 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
