Mbeya. Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Beno Malisa, amewataka wataalamu wa Nyanda za Juu Kusini kutafuta suluhu ya migogoro ya ardhi kwa kuimarisha usimamizi na upimaji wa maeneo ya wananchi.
Vilevile, wananchi wa mikoa hiyo wameombwa kujitokeza kwa wingi katika Maonesho ya Nanenane yanayofanyika jijini humo, ili kujifunza teknolojia mpya za kilimo, mifugo na uvuvi.
Akizungumza leo Agosti 1 wakati wa uzinduzi wa maonesho ya wakulima wa Nyanda za Juu Kusini, Malisa amesema njia ya kuondokana na migogoro ya ardhi ni kuwa na usimamizi imara na upimaji wa maeneo ya wananchi.
Pia ameshauri kuwepo matumizi sahihi ya viuatilifu, utunzaji wa mazingira, usimamizi wa usalama wa chakula na kutenga maeneo maalumu katika halmashauri zote, kwa ajili ya kuwawezesha vijana kupitia programu ya Jenga Kesho iliyo Bora (BBT).
"Mfano, Halmashauri ya Chunya imeshaanza. Tufuate mfano huo. Lakini kwa wananchi wa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, jitokezeni kwa wingi katika maonesho haya kujifunza teknolojia mbalimbali za kilimo, ufugaji na uvuvi.
"Lakini zipo fursa nyingi ambazo zikitumika vyema zinaweza kuleta tija, ikiwamo uwekezaji. Niziombe TFRA na TOSCI kuhakikisha mbegu zinapatikana kwa wakati kwa wananchi," amesema Malisa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Songwe, Jabir Makame, amewataka wananchi kutumia maonesho hayo kujifunza teknolojia mpya kwa kuzingatia kaulimbiu ya 'Tambua Soko, Ongeza Tija, Tekeleza Dira ya Maendeleo 2050.'
"Tutumie siku hizi za maonyesho kujifunza kuhusu masoko na teknolojia zitakazotusaidia kuongeza tija na kufikia Dira ya Maendeleo ya 2050, ambayo mafanikio yake yanatutegemea sisi wananchi," amesema.
Akitoa taarifa ya maonesho hayo kwa niaba ya makatibu tawala wa Nyanda za Juu Kusini, Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Rodrick Mpogolo, amesema hadi kufikia leo Agosti 1, jumla ya washiriki wa maonesho hayo wamefikia 242 kutoka katika kongani mbalimbali.
Amesema maonesho hayo yamekuwa chachu ya maendeleo kwa wananchi, wakiwamo wakulima, wafugaji na wavuvi, kupitia kujifunza na kushuhudia teknolojia mbalimbali katika mnyororo wa thamani wa sekta hizo.
"Waoneshaji 242 kutoka katika kongani za kampuni, taasisi za umma, vyuo, zana za kilimo, wajasiriamali na wafanyabiashara wameshiriki maonesho haya. Tunatarajia ushiriki mkubwa zaidi wa wananchi katika maonesho haya.
"Serikali inaendelea kuwawezesha wakulima kuhakikisha wanafanya shughuli zao kwa tija kwa kutenga bajeti ya Sh1.1 trilioni kwa ajili ya kuendeleza sekta ya kilimo katika msimu wa 2026/27 na Sh433.3 bilioni kwa sekta ya mifugo na uvuvi. Tunaamini hatua hiyo italeta matokeo chanya katika sekta hizo," amesema Mpogolo.
Mmoja wa wananchi na mjasiriamali, Shelida Msukwa, amesema matarajio yao ni kuonesha na kujifunza mbinu mbalimbali, akieleza kuwa maonesho hayo yanaweza kuifanya Serikali kuwatambua wabunifu na kuwafungulia fursa.
"Mimi ni mhitimu wa elimu ya biashara, lakini kwa kuwa sina mtaji wa kuanzisha biashara kubwa, nimeamua kujishughulisha na ujasiriamali wa miche na mboga mboga. Naiomba Serikali ituangalie na kututengenezea mazingira wezeshi," amesema Shelida.

Back to Home
RC Malisa: Pimeni mashamba kumaliza migogoro ya ardhi Nyanda za Juu Kusini
Mwananchi about 4 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
