Dar es Salaam. Serikali imeanza mchakato wa kupitia upya Sera ya Sayansi na Teknolojia kwa lengo la kuifanyia maboresho au kuandaa sera mpya itakayojumuisha masuala ya ubunifu.
Hatua hiyo inalenga kuimarisha mazingira ya kukuza bunifu na kuhakikisha sera hiyo inaendana na mabadiliko ya teknolojia duniani.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda ametoa kauli hiyo leo Alhamisi, Julai 30, 2026, katika ofisi ndogo za wizara hiyo Magogoni, jijini Dar es Salaam wakati akitangaza maandalizi ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu ya mwaka 2026, itakayofanyika katika Shule ya Sekondari Usagara, jijini Tanga, kuanzia Agosti 15 hadi 24.
Profesa Mkenda amesema sera iliyopo imepitwa na wakati kutokana na mabadiliko ya sayansi, teknolojia na ubunifu, hivyo Serikali inalenga kuwa na mfumo utakaosaidia si wabunifu mmoja mmoja pekee, bali mnyororo mzima wa ubunifu kuanzia ukuzaji wa mawazo hadi bidhaa kufika sokoni.
“Tunaipitia sera ya sayansi na teknolojia na baadaye tutaomba ifanyiwe marekebisho makubwa au kuandaa sera mpya ambayo inaweza kuitwa Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu,” amesema.
Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Profesa Carolyne Nombo amesema uhuishaji wa sera hiyo utaipa nchi mwongozo unaoendana na mazingira ya sasa, huku ukielekeza namna ya kusimamia maendeleo ya sayansi, teknolojia na ubunifu.
Akizungumza na Mwananchi, Mchumi wa Kidijitali, Francis Nyonzo amesema mafanikio ya sera hiyo yatategemea uwezo wake wa kujenga utamaduni wa kujifunza unaowawezesha wabunifu kuendelea kukuza maarifa yao kwa muda mrefu.
Amesema ubunifu haujengwi kwa muda mfupi, bali huanza kwa kuandaa watoto kupitia mfumo wa elimu na uwekezaji katika miundombinu inayowezesha tafiti na uvumbuzi.
Wakati huohuo, Serikali imewahimiza Watanzania kutumia bidhaa na huduma zinazotokana na ubunifu wa ndani ili kuongeza thamani ya kazi za wabunifu na kuchochea ukuaji wa viwanda vya ndani.
Pia, imeandaa mwongozo utakaohakikisha bidhaa za wabunifu wa Kitanzania zinapewa kipaumbele.
Mkurugenzi wa Sayansi, Teknolojia na Ubunifu katika wizara hiyo, Profesa Ladislaus Mnyone amesema Serikali imeidhinisha mkakati wa kuwashirikisha Watanzania wanaoishi nje ya nchi (diaspora) katika kutafuta fursa za maendeleo kwa wabunifu wa ndani.
Amesema Serikali pia imeanzisha madawati ya sayansi, teknolojia na ubunifu katika halmashauri ili kurahisisha utambuzi na uendelezaji wa bunifu na hadi sasa halmashauri 90 zimeanzisha madawati hayo.
Kupitia utaratibu huo, wabunifu wanaweza kuwasilisha mawazo yao na kuunganishwa na Tume ya Sayansi na Teknolojia pamoja na wadau wengine kwa ajili ya kupata msaada wa kitaalamu na kibiashara.
Profesa Mkenda amesema maadhimisho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yatawakutanisha taasisi za elimu, watafiti, wabunifu, sekta binafsi na wadau wengine kujadili maendeleo ya sekta hiyo.
Amesema pia kutafanyika mashindano ya Makisatu yaliyosaidia kuzalisha bunifu mbalimbali zikiwamo mashine ya kukamua mafuta ya parachichi, mabegi yenye mfumo wa sola, viti mwendo vya watu wenye ulemavu na mita janja za maji.

Back to Home
Sera mpya ya sayansi, teknolojia itakavyowasaidia wabunifu nchini
Mwananchi 1 day 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
