Dodoma. Serikali ya Jamhuri ya Korea, kupitia Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA), imetoa Sh9 bilioni kwa ajili ya kusaidia mradi wa kuboresha huduma za maji na kupunguza upotevu wa maji katika Wilaya ya Bahi, Dodoma.
Mradi huo wa msaada umezinduliwa leo, Ijumaa, Agosti 21, 2026, na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Mwajuma Waziri, ambaye amesema unatarajiwa kunufaisha wananchi 437,200 wa Bahi Sokoni, Kijiji cha Mpalanga na Dodoma Mjini.
Kupitia mradi huo, Serikali inalenga kuweka mfumo wa kisasa wa kudhibiti na kupunguza upotevu wa maji ili kuhakikisha kila tone la maji linalozalishwa linamfikia mlengwa.
Akizungumza wakati wa uzinduzi na makabidhiano ya mradi huo, Waziri amesema fedha hizo zimetolewa kama msaada kutokana na ushirikiano uliopo kati ya Tanzania na Jamhuri ya Korea katika kusaidia taifa kutekeleza malengo yake ya maendeleo, hususan katika sekta ya maji.
Amesema moja ya maeneo ambayo Serikali inayapa kipaumbele ni kuongeza ufanisi wa huduma za maji na kupunguza upotevu ambao kwa sasa umefikia asilimia 33.7.
“Ningependa kusisitiza kwamba Serikali inataka kila mradi unaotekelezwa kwa fedha za Serikali au kwa ushirikiano na washirika wa maendeleo uzingatie misingi ya uwazi, uwajibikaji, ubora, uadilifu na matumizi bora ya fedha. Hapa tunalenga kuzuia upotevu wa maji, lazima tufanikishe hilo,” amesema.
Aidha, amewaomba wananchi wa Bahi Sokoni, Ibihwa na Mpalanga kushirikiana na Serikali na taasisi zinazohusika ili kuhakikisha mradi huo unatekelezwa kwa ufanisi na kufikia malengo yaliyowekwa.
Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Dodoma (Duwasa), Aron Joseph, amesema mradi huo ulianza mwaka 2023 na unatarajiwa kukamilika mwaka 2028.
Amesema kati ya wananchi 437,200 watakaonufaika, takribani 410,000 ni wakazi wa Dodoma Mjini, huku 27,000 wakiwa wakazi wa vijiji vya Wilaya ya Bahi.
Kwa upande wa Bahi Sokoni, amesema mradi utahusisha uendelezaji wa miundombinu, uboreshaji wa visima viwili vya maji, usimikaji wa pampu za kuvutia maji pamoja na ujenzi wa mabomba ya kusafirisha maji kwa umbali wa kilomita 19.
Katika Kijiji cha Mpalanga, amesema kutajengwa kilomita 8.6 za mabomba mapya pamoja na vituo vitano vya kuchotea maji.
Balozi wa Jamhuri ya Korea nchini Tanzania, Eun Ju Ahn, amesema mradi huo unalenga kuwa suluhisho la tatizo la upotevu wa maji na kupunguza gharama za uendeshaji wa huduma hiyo.
Amesema mfumo huo utasaidia kuhakikisha kila tone la maji linahesabiwa na kufuatiliwa katika mchakato wa uzalishaji na usambazaji.
Kwa mujibu wa Balozi Eun, mradi huo pia utahusisha usimikaji, ufungaji, upimaji na uanzishaji wa mfumo wa Wireless SCADA (Supervisory Control and Data Acquisition) utakaowezesha ufuatiliaji wa miundombinu ya maji kwa njia ya kidijitali.
Amesema mfumo huo utamwezesha mtumishi mmoja kufuatilia hali ya usambazaji wa maji na kubaini kwa haraka kisima au sehemu ya mtandao ambayo haifanyi kazi, badala ya kutegemea idadi kubwa ya watumishi kufanya ufuatiliaji huo.
Amesema pia wataalamu wa Tanzania watapatiwa ujuzi wa kiufundi ambao unaweza kutumika katika maeneo mengine.

Back to Home
Sh9 bilioni kunufaisha wananchi 437,200 mradi wa maji Bahi
Mwananchi about 3 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
