Tanga.Wilaya ya Tanga imeanza kuchukua hatua za tahadhari kwa kutembelea na kutambua maeneo yote hatarishi yanayoweza kuathiriwa na mvua za El Niño, ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuzuia madhara yanayoweza kusababishwa na mvua hizo ambazo zimetabiriwa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).
Idara mbalimbali zimeanza kutembelea maeneo tofauti katika Wilaya ya Tanga, zikiongozwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya hiyo, kwa lengo la kubaini changamoto zilizopo na kukubaliana kwa pamoja hatua za kuchukua kulingana na hali ya kila eneo.
Mkuu wa Wilaya ya Tanga, Dadi Kolimba, amesema Serikali haitaki kuona mvua hizo zikiambatana na madhara kwa wananchi, hivyo maandalizi yameanza ili kuhakikisha wananchi wanapita katika kipindi hicho kwa usalama.
Kolimba amesema wilaya hiyo imeanza kujipanga mapema, huku ikitekeleza maelekezo yaliyotolewa na Rais Samia Suluhu Hassan ya kuchukua tahadhari dhidi ya mvua hizo kabla hazijaanza na kusababisha madhara.
“Sisi leo pamoja na Kamati ya Ulinzi na Usalama na viongozi wengine wa maeneo ya mitaa tumeamua kupita na kutambua maeneo ambayo ni hatarishi, ambayo mvua zikianza kunyesha yanaanza kujaa maji. Tulianza kuyatambua tukiwa ndani kwenye mkutano wa kawaida, na sasa tunapita field kuangalia maeneo yenyewe na kupeana majukumu,” amesema Kolimba.
Amesema zoezi hilo limehusisha Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Tanga (Uwasa), Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (Tarura), Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads) pamoja na Halmashauri ya Jiji la Tanga.
Kwa mujibu wa Kolimba, baada ya maeneo hatarishi kutambuliwa, kila taasisi itapewa jukumu la kutekeleza hatua zinazohitajika, ikiwemo kuboresha miundombinu na kuziondoa changamoto zinazoweza kusababisha mafuriko.
Amesema baada ya muda watapita tena katika maeneo hayo kukagua utekelezaji wa majukumu waliyopeana na kuona kama maelekezo yaliyotolewa yametekelezwa.
Kwa upande wake, Kaimu Mkurugenzi wa Jiji la Tanga, Sebastian Danda, amesema moja ya changamoto kubwa iliyopo jijini humo ni mifereji mingi kuziba, hali inayoweza kusababisha maji ya mvua kushindwa kupita katika njia zake na hivyo kuingia kwenye makazi ya wananchi.
Amesema hatua za kukabiliana na changamoto hiyo zinapaswa kuchukuliwa mapema kabla ya mvua kuanza, kwa kuwa wakati mvua zinapokuwa zimenyesha kwa wingi inakuwa vigumu kufanya usafi na kuzibua mifereji.
“Tunatakiwa kufanya kwa haraka zoezi hilo kabla ya mvua kuanza, kwa kuwa mvua zikishaanza hatutaweza kupata fursa ya kuzibua mifereji wakati maji yapo. Kwa hiyo sasa tunaanza kuangalia ile miundombinu ili hata kama maji yakija, hata yakiwa mengi kiasi gani, yaweze kuondoka haraka kwenye makazi ya watu ili mafuriko yasiweze kutokea,” amesema Danda.
Naye Mwenyekiti wa Mtaa wa Usagara A, Kata ya Usagara jijini Tanga, Shabani Msheri, amesema hatua hiyo ni muhimu kwa kuwa itasaidia kuwaepusha wananchi na adha ya mafuriko ambayo wamekuwa wakikumbana nayo katika maeneo korofi wakati wa mvua.
“Naipongeza Serikali kwa kuliona hili, kwa kuwa limekuwa ni kero kubwa sana kwenye mtaa wangu. Hali hiyo inasababisha madhara kwa watembea kwa miguu ambao wanashindwa kupita kwenye baadhi ya maeneo,” amesema Msheri.

Back to Home
Tanga yaanza kazi kutambua maeneo hatarishi kukabiliana na mvua za El Niño
Mwananchi 1 day 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
