Dar es Salaam. Tanzania imepiga hatua katika kuimarisha mifumo ya kukabiliana na utakatishaji fedha haramu, ufadhili wa ugaidi na ufadhili wa silaha za maangamizi.
Mafanikio haya yanashuhudiwa wakati ambao serikali imeweka bayana kuwa bado inaendelea kushughulikia maeneo 15 yaliyoainishwa katika tathmini ya kimataifa ikiwemo ikiwemo marekebisho ya sheria 12 zilizobainishwa kuwa zinahitaji maboresho kwa upande wa Tanzania Bara na Zanzibar.
Waziri wa Fedha, Balozi Khamis Mussa Omar ameyasema hayo jana jijini Kigali, Rwanda, wakati wa Mkutano wa 26 wa Baraza la Mawaziri la Umoja wa Nchi za Mashariki na Kusini mwa Afrika wa Kupambana na Utakasishaji Fedha Haramu, Ufadhili wa Ugaidi na Silaha za Maangamizi (ESAAMLG).
Amesema Tanzania imefanikiwa katika tathmini ya pamoja iliyofanywa na ESAAMLG kupitia Kamati ya Wataalamu huku Serikali ikiendelea kutekeleza maboresho yaliyobainishwa ili kuimarisha sekta ya fedha na kusaidia maendeleo ya kiuchumi na kijamii.
“Tuna sheria na kamati ya kitaifa ya kupambana na masuala haya. Mafanikio ni makubwa lakini bado kuna maeneo 15 tunayafanyia kazi ikiwemo marekebisho ya sheria 12 zilizobainishwa kuwa zinahitaji maboresho kwa upande wa Tanzania Bara na Zanzibar,” amesema.
Kati ya maeneo hayo, Tanzania Bara tayari imepitisha sheria nne kupitia Bunge katika kikao kinachoendelea huku Serikali ya Mapinduzi Zanzibar ikitarajiwa kuwasilisha miswada ya marekebisho ya sheria nyingine tatu.
Amesema hatua hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mapendekezo yaliyotolewa baada ya tathmini ya mifumo ya Tanzania ya kuzuia na kukabiliana na uhalifu wa kifedha.
Amesema mafanikio hayo yametokana na ushirikiano wa taasisi mbalimbali za Serikali, zikiwemo Wizara ya Fedha, wasimamizi wa sekta ya benki, Wizara ya Katiba na Sheria, Wizara ya Mambo ya Ndani na taasisi nyingine zinazounda Kamati ya Kitaifa ya kupambana na utakasishaji fedha haramu na vitendo vinavyohusiana.
“Kuimarishwa kwa mifumo hiyo ni muhimu katika kulinda sekta ya fedha dhidi ya fedha zinazotokana na uhalifu na kuhakikisha Tanzania inaendelea kuwa na mfumo unaokidhi viwango vya kimataifa,’ amesema.
Mkutano huo wa Kigali umewakutanisha mawaziri, makatibu wakuu na maafisa waandamizi kutoka nchi wanachama wa ukanda wa Mashariki na Kusini mwa Afrika kwa ajili ya kujadili namna ya kuimarisha ushirikiano katika mapambano dhidi ya utakasishaji fedha haramu, ufadhili wa ugaidi na ufadhili wa silaha za maangamizi.
Kutoka Tanzania, viongozi walioshiriki ni Waziri wa Katiba na Sheria, Dk Juma Homera, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dk Seif Abdallah Shekalaghe, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha na Mipango-Zanzibar, Aboud Hassan Mwinyi na Kamishna wa Kitengo cha Ujasusi wa Fedha (FIU), Majaba Magana.
Wengine ni Naibu Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kitaifa ya Wataalamu ya Kuzuia Utakatishaji Fedha Haramu, Sauda Msemo pamoja na wakuu wa taasisi, wataalamu wa sekta ya fedha, wasimamizi wa taasisi za kifedha na wadau wa maendeleo.
Mkutano huo pia unalenga kuimarisha ushirikiano wa nchi wanachama katika kubadilishana taarifa na uzoefu wa kukabiliana na uhalifu wa kifedha unaoweza kuhatarisha uchumi, usalama na mifumo ya fedha ya nchi.

Back to Home
Tanzania yapiga hatua mapambano utakatishaji fedha
Mwananchi about 2 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
