Kahama. Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kikodi Kahama, kwa kushirikiana na Mamlaka ya Dawa na Vifaa Tiba (TMDA), imeteketeza shehena ya sigara zaidi ya milioni 11.4 aina ya Supermatch King Size Filter, iliyokamatwa katika Bandari Kavu ya Isaka mkoani Shinyanga mwaka 2024.
Shehena hiyo iiyokuwa ikiingizwa nchini kwa njia ya magendo, ilikuwa na katoni 2,295 kila moja ikiwa na sigara 5,000, sawa na jumla ya sigara 11,475,000 zenye thamani ya zaidi ya Sh2.2 bilioni.
Shehena hiyo ilikuwa imebebwa na kontena lenye namba ZG 7255, likitokea Burundi na kudaiwa kuingizwa nchini kinyume cha sheria.
Akizungumza leo Agosti 29, 2026 wakati wa shughuli ya uteketezaji huo, Meneja wa TRA Mkoa wa Kahama, Wilson Kamwamu amesema shehena hiyo ilikamatwa baada ya mamlaka hiyo kupata taarifa za ndani, ambapo vibali vilionyesha ni pumba lakini baada ya ukaguzi ikagundulika ni sigara feki.
“Mwaka 2024 tulikamata huu mzigo ukitokea Burundi. Taarifa zetu za awali zilionyesha kuwa huu mzigo ulikuwa unapita kuelekea transit na vibali vyake vilionyesha umebeba pumba lakini baada upekuzi tukagundua ni shehena za sigara” amesema.
Amesema baada ya kukamatwa mamlaka hiyo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ilifanya uchunguzi ili kuthibitisha uhalali na usalama wa bidhaa hizo, ndipo zilipogundulika kuwa sio salama kwa matumizi ya binadamu.
Amesema endapo sigara hizo zingefanikiwa kuingizwa sokoni, TRA ingepoteza mapato ya zaidi ya Sh1.6 bilioni.
Kwa mujibu wa Kamwamu, baada ya shughuli ya uteketezaji wa sigara hizo, wataendelea na jitihada za kuwapata wahusika ambao mpaka sasa hawajajitokeza, kabla ya gari ya mzigo kutaifishwa.
“Lengo letu kubwa ni kupeleka ujumbe kwa wenzetu wafanyabiashara kwamba magendo siyo kitu kizuri, yanaathiri uchumi, mitaji na hata athari zipo kubwa pia kwa watumiaji,” mesema Kamwamu.
Meneja wa TMDA Kanda ya Ziwa Magharibi, Dk Edgar Mahundi amesema mamlaka hiyo kupitia wataalamu wake ilichukua sampuli za sigara hizo na kuzipeleka maabara wa ajili ya vipimo na ndipo ilipogundulika kuwa si salama kwa matumizi ya binadamu.
“TRA walitaka uthibitisho kutoka kwetu kama ni salama tulipeleka maabara na kuthibitisha kwamba sigara hizi zina kemikali, zina kiwango cha kemikali kinachozidi viwango vya kimataifa, kwa hiyo moja kwa moja tukaamua kwamba sigara hizi hazifai kwa matumizi ya binadamu,” amesema Mahundi.
Amesema endapo kama zingewafikia watumiaji zingesababisha madhara ikiwemo kuongeza hatari ya kupata saratani ya mapafu, figo na ini kwa watumiaji zaidi ya 11,475,000.
“Madhara moja kwa moja kama sigara hizi zingeenda moja kwa moja kwenye matumizi ya watanzania, maana yake kemikali zilizomo katika sigara wakati mtumiaji anapovuta zinaweza kusababisha saratani ya mapafu, figo na ini,” amesema.
Akieleza madhara mengine, Mahundi amesema kemikali hizo zinapoingia katika mzunguko wa damu zinaweza kuathiri viungo mbalimbali vya mwili, ikiwemo ubongo hali inayoweza kusababisha changamoto ya afya ya akili na athari katika mfumo wa uzazi.
“Zikifika zikakaa kwenye ubongo, utagundua mtu anaanza kuonyesha dalili za kupoteza fahamu, lakini zinasababisha madhara ya matatizo ya afya ya akili, zinapozunguka zikaenda kwenye via vya uzazi, kwa mwanaume wanaweza kushindwa kutengeneza mbegu, lakini kwa mwanamke kushindwa kubeba mimba,” ameongeza.
Aidha, amewataka wafanyabiashara na wananchi kuwa makini katika kuhakikisha bidhaa za tumbaku zinakidhi matakwa ya kisheria kabla ya kumfikia mlaji wa mwisho.
“Sigara hizi kabla zijaingizwa kwenye soko la Tanzania zinatakiwa zihifadhiwe kwa mujibu wa sheria. Niwaombe Watanzania wanaotumia sigara wajiridhishe na nembo zilizomo kwenye sigara, ikiwemo nembo ya TRA,” amesema.

Back to Home
TRA, TMDA wateketeza sigara feki zenye thamani ya Sh2.2 bilioni
Mwananchi about 3 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
