Dar es Salaam. Wanachama wa Jumuiya ya Wasioona Tanzania (TAB) wameiomba Serikali kuweka mpango maalumu wa kutoa mafunzo ya muda mrefu kuhusu sheria na usalama barabarani ili kuwawezesha kuendesha maisha yao kwa uhuru na usalama zaidi.
Ombi hilo limetolewa na mlezi wa jumuiya hiyo, James Shimwenye wakati wa mafunzo maalumu ya usalama barabarani yaliyoandaliwa kwa wanachama wa TAB kwa kushirikiana na Taasisi ya Mpango wa Usalama Barabarani (Tarsi).
Akizungumza leo Jumatano, Mei 20, 2026 katika mafunzo hayo, Shimwenye amesema licha ya mafunzo hayo kuwa ya siku moja, yamekuwa na umuhimu mkubwa kwa wasioona ambao hukutana na changamoto nyingi wanapotumia barabara katika majiji makubwa kama Dar es Salaam.
Shimwenye amesema changamoto kubwa ni ukosefu wa alama maalumu zinazoweza kuwasaidia kutambua mazingira ya barabarani ikiwemo maeneo salama ya kuvuka, pamoja na namna ya kutambua taa za kuongozea magari zinaporuhusu au kuzuia watumiaji wa barabara kuvuka.
“Wengi wetu tunatumia fimbo nyeupe kama alama yetu, lakini bado madereva wengi hawatambui umuhimu wake. Hali hii husababisha kusubiri muda mrefu kabla ya kupata msaada wa kuvuka barabara,” amesema.
Changamoto nyingine amesema ni baadhi ya vyombo vya usafiri kutosimama vizuri katika vituo, jambo linalowasababishia usumbufu mkubwa wanapopanda au kushuka.
Mkurugenzi wa Tarsi, Maliki Barongo amesema ipo haja ya kuwajengea uwezo watu wenye ulemavu wa macho kuhusu matumizi salama ya barabara ili kupunguza ajali zinazoweza kuzuilika.
Amesema kundi hilo limekuwa likisahaulika katika utoaji wa elimu ya usalama barabarani licha ya kuwa ni miongoni mwa watumiaji wa barabara walio katika hatari kubwa ya kupata ajali.
“Tumekuwa tukiona elimu ya usalama barabarani ikitolewa kwa makundi mbalimbali ya watumiaji wa barabara, lakini watu wenye ulemavu wa macho wamekuwa wakisahaulika. Kupitia mafunzo haya tunaamini wataweza kujitambua, kujilinda na kusaidia kupunguza ajali za barabarani,” amesema Barongo.
Mkuu wa dawati la elimu kwa umma kutoka makao makuu ya kikosi cha usalama barabarani, Mbunja Matibu amewataka madereva wa vyombo vya moto nchini kuzingatia alama za watu wenye ulemavu wa kuona na kupunguza mwendo wanapofika maeneo ya vivuko ili kuepusha ajali zinazoweza kuzuilika.
Mbunja amesema watu wenye ulemavu wa kuona wanahitaji ushirikiano kutoka kwa watumiaji wengine wa barabara ili waweze kuvuka kwa usalama kutoka upande mmoja kwenda mwingine.
“Madereva wanapaswa kupunguza mwendo na inapobidi kusimama kabisa ili kumpa nafasi mtu mwenye ulemavu kuvuka barabara kwa usalama na wanapaswa kutambua alama zinazoonyesha watu wenye changamoto ya kuona au kusikia,” amesema.
Mwanafunzi wa Chuo cha Ufundi na Marekebisho, Winfrida Baltazar ameishauri Serikali kuendelea kutoa elimu ya usalama barabarani kwa watu wenye ulemavu wa kuona ili kuwasaidia kutumia barabara kwa usalama zaidi.
Amesema mafunzo ya usalama barabarani yaliyotolewa kwa watu wenye ulemavu wa kuona imekuwa muhimu kwa kuwa itawasaidia kutambua namna bora ya kujilinda wanapokuwa barabarani.
"Washiriki wa mafunzo haya wako tayari kuwa mabalozi wa kueneza elimu waliyoipata kwa watu wengine wenye ulemavu wa kuona ambao hawakupata nafasi ya kushiriki," amesema Winfrida.