Dodoma. Serikali imetakiwa kuwekeza nguvu katika umaliziaji wa miradi ya zamani kabla ya kuanzisha miradi mipya licha ya uwepo wa mahitaji.
Ushauri huo umetolewa leo Jumatatu Mei 18, 2026 na Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu, Seleman Kakoso wakati wa utiaji saini wa mradi wa ujenzi wa barabara ya njia sita kutoka katikati ya Jiji la Dodoma hadi njiapanda ya Chamwino yenye urefu wa kilomita 32.
Mradi huo umesanifiwa kwa jina ‘mradi wa usafiri jumuishi na endelevu katika Jiji la Dodoma’ (Dodoma Integrated and Sustainable Transport Project” (DIST).
Kakoso amesema ni wakati sasa Serikali kuweka kipaumbele miradi yote ya viporo hata kama kutakuwa na miradi mipya lakini nguvu ielekezwe miradi ya zamani kwani mingi imesimama.
Mradi utatekelezwa kwa kipindi cha miezi 36 na Kampuni ya M/s China Railway Construction Engineering Group Co. Ltd (CRCEG) ya China kwa gharama ya Sh269 bilioni inayojumuisha na ulipaji wa fidia.
Kwenye ujenzi huo, mradi utahusisha barabara za kutoka Dodoma Mjini hadi Njiapanda ya Chamwino, Dodoma Mjini hadi Njiapanda ya Msalato na kutoka Dodoma mjini (mzunguko wa Image kituo cha reli ya mwendokasi (SGR Station), Mkonze.
Katika taarifa iliyotolewa na wizara, mradi unajumuisha taasisi mbalimbali ikiwamo Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroads), Wakala wa Barabara za Mijini na Vijijini (Tarura), Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Ardhini (Latra) na Halmashauri ya Jiji la Dodoma ambapo Tanroads ndiyo kiongozi katika uratibu wa utekelezaji wake.
Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Mkuu wa Wilaya ya Dodoma, Alhaji Jabiri Shekimweri ameomba ujenzi wa mradi huo uzingatie matoleo kwa wapita njia kwani barabara hiyo inagusa maeneo yenye watu wengi ili kuepuka ajali.
Akijibu hoja hizo, Waziri wa Ujenzi, Abdallah Ulega amekiri kwa uwepo wa ajali nyingi katika maeneo ya kutoka eneo la Kimbinyiko hadi Kituo cha Kisasa, hivyo akaelekeza ombi la mkuu wa wilaya lifanyiwe kazi ikiwamo kuweka taa zenye uwezo mkubwa.
Waziri Ulega amesema ndani ya barabara hiyo zitatengenezwa bustani nzuri zenye kuvutia ili eneo hilo lisifanane na barabara ya kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere jijini Dar es Salaama ambayo amesema haina mvuto.
Kuhusu ukamilishwaji wa miradi ya zamani, amesema wazo hilo wanalifanyia kazi na kwa sasa hawatakubali kuona miradi inapoa.