Dodoma. Mkutano wa nne wa Bunge la 13 unatarajiwa kuanza Jumatano, Agosti 26, 2026, huku macho na masikio ya Watanzania yakielekezwa kwenye miswada mitatu, pamoja na taarifa za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) zinazotarajiwa kujadiliwa.
Miswada hiyo ni Muswada wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 2 wa mwaka 2026, Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Kilimo na Muswada wa Sheria ya Kufuta Tasnia ya Pareto wa mwaka 2016.
Miswada hiyo imepelekwa katika Kamati za Kudumu za Bunge kwa uchambuzi, ikiwamo Kamati ya Katiba na Sheria, pamoja na Kamati ya Viwanda, Biashara, Kilimo na Mifugo.
Miongoni mwa masuala yanayotarajiwa kuibua mjadala ni marekebisho ya sheria inayohusu utaifishaji wa mifugo inayokutwa ndani ya hifadhi, ambayo imekuwa ikilalamikiwa na baadhi ya wadau kwa muda mrefu.
Itakumbukwa, Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba, alipokuwa akihitimisha Mkutano wa Tatu wa Bunge, alisema moja ya mambo yatakayofanyika katika marekebisho ya sheria mbalimbali ni kuibadili sheria hiyo.
Alisema mchakato wa marekebisho umepitia hatua mbalimbali na kilichobaki ni kuufikisha muswada Bungeni kwa ajili ya kujadiliwa na kufanyiwa marekebisho, akieleza kuwa sheria hiyo imeonekana kuwa kandamizi.
Sheria hiyo imekuwa chanzo cha malalamiko miongoni mwa wafugaji wanaodai baadhi ya mifugo yao imekuwa ikikamatwa kwa madai ya kuingia katika maeneo ya hifadhi, huku wengine wakilalamikia utaratibu wa utaifishaji.
Akizungumza na Mwananchi leo Jumatatu, Agosti 24, 2026, mfugaji, Petro Ole Lemomo, amesema pamoja na kufanya marekebisho, Bunge linapaswa kuangalia kwa kina kipengele cha utaifishaji, pamoja na gharama zinazotozwa, ili kuepusha mianya ya baadhi ya watu kutumia sheria hiyo kuwaonea wafugaji.
“Nakubali kwamba inaweza kuwa jambo jema kuondoa utaifishaji, lakini ikaacha malipo makubwa kwa mfugo mmoja, ambayo haitakuwa na utofauti kwenye utaifishaji, maana janjanja ni nyingi,” amesema.
Kwa mujibu wa ratiba ndogo iliyotolewa na Ofisi ya Bunge, ratiba kamili ya shughuli za mkutano huo inatarajiwa kutolewa Jumatano mchana.
Mbali na miswada hiyo, mkutano huo unatarajiwa kuwa wa kwanza kwa Bunge la 13, chini ya Spika Mussa Zungu, kujadili taarifa za CAG tangu uchaguzi mkuu ulipofanyika Oktoba 29, 2025.
Kwa mujibu wa utaratibu wa Bunge, mkutano wa kwanza baada ya mkutano wa bajeti huwa na nafasi ya kujadili marekebisho ya sheria mbalimbali, pamoja na taarifa za CAG.
Dalili za mjadala huo zimeanza kuonekana katika vikao vya Kamati za Bunge, ambako Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC), chini ya Mwenyekiti wake, Ado Shaibu, imekataa taarifa ya Halmashauri ya Wilaya ya Same kwa madai ya kutokuwa tayari kujibu hoja za ukaguzi.
Kamati ya Hesabu za Serikali Kuu (PAC), chini ya Mwenyekiti wake, Devotha Minja, nayo imehoji hesabu za Wakala wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) na Chuo Kikuu cha Mzumbe, ikieleza kuwa baadhi ya taarifa zilikuwa na utata na kutaka taasisi hizo kujitafakari.
Hali hiyo inaashiria kuwa ripoti za CAG zinaweza kuwa miongoni mwa hoja zitakazotawala mjadala wa Bunge, huku wabunge wapya wakikabiliwa na mtihani wa kuonyesha namna watakavyowakilisha wananchi kuhusu matumizi ya fedha za umma na hoja za ukaguzi katika maeneo yao.
Mbunge wa Tunduru Kaskazini (ACT-Wazalendo), Ado Shaibu, amesema mkutano huo ni fursa ya wabunge kuwasilisha hoja za wananchi na kwamba atatumia nafasi hiyo kutetea masuala yanayowahusu wananchi.
Ado amekuwa miongoni mwa wabunge walioonekana mara kwa mara wakichangia katika vikao vilivyopita, huku akisisitiza kuwa wabunge wanapaswa kutumia nafasi zao kuwasemea wananchi.
Kwa upande wake, mmoja wa wabunge wa muda mrefu kutoka Dodoma, amesema mjadala wa ripoti za CAG si jambo jipya kwa Bunge, kwa kuwa umekuwa sehemu ya shughuli zake za kawaida.
Hata hivyo, amesema uzalendo na msimamo wa Spika Zungu katika kusimamia mali za umma unaweza kuufanya mkutano huo kuwa na sura tofauti na kuwapa wabunge nguvu zaidi katika kujadili hoja za matumizi na usimamizi wa fedha za umma.

Back to Home
Miswada mitatu kujadiliwa mkutano wa nne wa Bunge
Mwananchi about 3 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
