Mbeya. Siku chache baada ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kuzindua mikutano yake mkoani Mbeya huku kikieleza changamoto zinazowakabili wananchi, Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoani humo kimesema kipo tayari kujibu kwa hoja maendeleo yaliyofanywa na Serikali.
Mei 10, 2026 Chadema ilizindua mikutano yake chini ya Mwenyekiti wa chama hicho Kanda ya Nyasa, Joseph Mbilinyi ‘Sugu’ mkutano uliofanyika Uyole jijini Mbeya, huku kikieleza kutoridhishwa na utendaji wa Serikali katika miradi mbalimbali ya maendeleo.
Mkutano huo ulioongozwa na Sugu pia ulihusisha viongozi mbalimbali akiwamo Mwenyekiti wa chama hicho Kanda ya Kusini, Bele Polila, Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Mbeya, Masaga Karolin na Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake Taifa, Elizabeth Mwakimomo.
Baada ya mkutano huo, chama hicho kiliendelea na mikutano yake katika wilaya zote za Mkoa wa Mbeya iliyohitimishwa jana Jumapili Mei 17 kwa lengo la kuzindua shughuli rasmi kwa ajili ya viongozi wa ngazi za chini kuendelea na kazi.
Hata hivyo, CCM mkoani humo imesema ipo tayari kujibu kwa hoja na vitendo kwa shughuli za maendeleo zilizofanywa na Serikali kupitia chama hicho, huku ikitaka kutanguliza uzalendo na amani ya nchi.
Hoja za Chadema
Akizungumza katika mkutano huo, Sugu alisema kwa sasa Serikali ni kama haiendi kwakukosa fedha za kuendesha miradi, akiitaja Mbeya kwenye eneo la barabara ya njia nne ambayo alieleza kusuasua kwake.
Pia, mbunge huyo wa zamani wa Mbeya mjini aligusia mradi wa maji kutoka Mto Kiwira akibainisha kuwa kwa sasa haoni kinachofanyika hadi wananchi kufikia hatua ya ‘kunuka kwapa.’
“Nchi imegoma kwenda kutokana na kukosa fedha, mfano hapa Mbeya maji ni shida na nilishasema suluhisho la tatizo hili ni mto Kiwira lakini hakuna kinachofanyika zaidi ya kupiga miruzi.”
“Barabara ya njia nne inasuasua hatuna mtu wa kusimamisha Shilingi njia zikajengwa, kwa sasa walichofanya ni kuharibu bora wangeacha barabara moja iliyokuwepo” alisema Sugu.
Mwenyekiti huyo alidai kuwa hawatasita kuendelea kuzungumza ukweli kuhusu maendeleo ya wananchi na kwamba kwa sasa umma umepoteza imani na matumaini kwa Serikali inayoongozwa na CCM.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama hicho Mkoa wa Mbeya, Masaga Karoli alisema kwa hali ya maisha ya wananchi ni magumu sana akikumbushia matukio ya vurugu za Oktoba 29 kuacha maumivu.
Naye Mwenyekiti wa Baraza la Vijana (Bavicha) mkoani Mbeya, Elisha Chonya alidai kwa sasa hakuna serikali inayoweza kuwajibisha mhimili wowote kwa kuwa wote ni wateule wa Rais.
Alisema kwa sasa Bavicha na Chadema kwa ujumla wanatarajia kuanza kutembea nyumba kwa nyumba, mtaa kwa mtaa na Kata kwa Kata kusikiliza kero za wananchi na kuzianika hadharani.
“Hakuna haki kwa kuwa kila mmoja ni mteule wa Rais, wanashindwa kuwajibishana, sisi Chadema na Bavicha tutaendelea kudai haki na maendeleo kwa wananchi na tumejipanga kupita mtaa, kata na nyumba kumfikia kila mmoja” alisema Chonya.
CCM yajibu
Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (MNEC) Mkoa wa Mbeya, Ndele Mwaselela alisema chama hicho kinafanya kazi kwa mujibu wa ilani akieleza kuwa wapo tayari kujibu hoja kwa vitendo.
Alisema katika ilani ya CCM imeanisha miradi ya utekelezaji ikiwamo miundombinu ya barabara, ufungaji taa 100 na kamera barabarani, vivuko vinavyounganisha kata kwa kata.
“Mfano Mbeya Mjini ilani ya chama Mkoa inaainisha ujenzi wa barabara, vivuko, ufungaji kamera, kuimarisha ulinzi na usalama, ujenzi wa madaraja, kwa hiyo tunao mpango wa kujenga njia za ndani zenye kilomita nyingi.
“Kuhusu barabara ya njia nne tayari mkandarasi amerejea kazini kwa ajili ya kuendelea na kazi na tumemtaka aongeze kasi ili amalize kwa wakati, tunajua changamoto iliyokuwapo ya vumbi tumeelekeza Tanroad amwage maji” amesema Mwaselela.
Kigogo huyo amesisitiza kuwa hakuna mradi wowote utakaosimama chini ya mwenyekiti wao ambaye ni Rais Samia Suluhu Hassan, akiwaomba wananchi kuendelea kukiamini chama hicho.
“Serikali ipo kazini, yapo mambo yatakayofanywa mwaka huu, mwakani na mwaka mwingine kwa kuwa hakuna kitu kilichoahidiwa na CCM kikashindwa kutekelezeka, tatizo wanaosema hawasomi ilani yetu.”
“Kama zipo changamoto zinazojitokeza zipo ngazi kuanzia chini zinatekeleza, tunataka Chadema wazunguke watuambie wapi penye kasoro ili tuwaoneshe tulichofanya kwa vitendo” amesema Mwaselela.
Amesema dhamira ya CCM ni kutekeleza na kutoa huduma bora kwa jamii akisisitiza kuwa Chadema wanapaswa kuhubiri amani ili wanachodai kiweze kupatikana kwa amani na kutanguliza utaifa kwanza.
Amesema kuwa haitawezekana iwapo maendeleo hayataambatana na amani badala yake itakuwa ni mzigo mzito zaidi kwa wananchi, akibainisha kuwa Chadema wanaipambania dola hivyo lazima waiseme CCM kwa ubaya.
“Wao pia (Chadema) ni Watanzania, waihubiri amani, CCM kazi yake ni kuleta maendeleo hakuna kazi inayosimama, unaona viongozi wa juu akiwamo Waziri Mkuu anazunguka nchini kusikiliza na kutatua kero.”
“CCM inachofanya ni kusimamia viongozi wa Serikali wakiwamo wabunge na madiwani kuhakikisha wanaweka mipango ya kuwahudumia wananchi, tunao wafuatiliaji na wanaotekeleza,” amesema MNEC huyo.
Amesisitiza CCM itaendelea kuisimamia Serikali na kwamba watakuwa makini kusikiliza dosari zinazoibuliwa na Chadema mkoani humo na kuhakikisha wanazitekeleza na kujibu hoja kwa vitendo.
Kwa upande wake Katibu wa Chama hicho, Mbeya Mjini, Mohamed Mavallah alisema mwenye macho haambiwi tazama akibainisha kuwa chama hicho kinajivunia maendeleo yaliyopo jijini Mbeya.
Amesema miradi mbalimbali ya maendeleo na huduma bora za kijamii ikiwamo vituo vya afya, hospitali na zahanati, barabara na shule ni baadhi ya mambo yaliyofanyika kwa ufanisi na wananchi wanafurahia huduma.
“Na sisi tunajipanga kujibu hoja zao kwa kuwaonyesha, hiyo ni haki yao kikanuni kutembea popote na hatutasita kuwajibu tulichokifanya na tunachoendelea kufanya, mfano barabara zinajengwa, huduma za afya zipo na shule zenye ubora” amesema Mavallah.