Dar es Salaam. Ni rasmi Jimbo la Chamwino mkoani Dodoma, lipo wazi baada ya aliyekuwa mbunge wake, Deogratius Ndejembi kupendekezwa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), kuwa Makamu wa Rais.
Kikao cha NEC kilichoketi Agosti 26, 2026 Dar es Salaam na kuongozwa na mwenyekiti wake Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kauli moja kimepitisha Ndejembi katika nafasi hiyo.
Ndejembi ambaye kabla ya kupendekezwa alikuwa Waziri wa Nishati, anachukua nafasi ya Dk Emmanuel Nchimbi aliyeomba kujiuzulu Jumanne Agosti 25, 2026 na ombi lake kuridhiwa na Rais Samia.
Kwa mujibu wa Katiba ya Tanzania Ibara ya 71(1) (e) inaeleza jinsi mbunge anavyoweza kukoma kuwa mbunge na ataacha kiti cha ubunge miongoni mwa sababu ni atachaguliwa au atateuliwa kuwa Makamu wa Rais.
Kwa maana hiyo, hatua itakayofuata kwa sasa ni Spika wa Bunge, Mussa Zungu kuijulisha Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) kuhusu jimbo la Chamwino kuwa wazi.
Baada ya hapo INEC itatangaza na kuanza taratibu za mchakato wa uchaguzi mdogo wa jimbo hilo, ambalo Ndejembi aliliongoza tangu mwaka 2020.

Back to Home
Rasmi Jimbo la Chamwino lipo wazi
Mwananchi about 2 hours 1 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
