Dar es Salaam. Watu 129 hawajulikani walipo nchini Indonesia baada ya meli ya abiria ya Virgo Transport 8 kupinduka katika Bahari ya Java, huku watu sita wakithibitishwa kufariki na 108 kuokolewa.
Kwa mujibu wa Reuters, ajali hiyo ilitokea Jumapili, Septemba 13, 2026, wakati meli hiyo ikiwa safarini kutoka Surabaya, Mashariki mwa Java, kuelekea Banjarmasin, Kusini mwa Kalimantan.
Meli hiyo ilikuwa imebeba watu 243, wakiwemo abiria 213 na wafanyakazi 30.
Reuters imeripoti kuwa meli hiyo ilipoteza mawasiliano na mamlaka karibu saa 2:00 asubuhi kwa saa za Indonesia baada ya kukumbwa na hali mbaya ya hewa baharini.
Baadaye iliripotiwa kuwa meli hiyo ilipinduka katika eneo la Masalembo, takribani kilomita 148 kutoka Banjarmasin.
Mkuu wa Wakala wa Kitaifa wa Utafutaji na Uokoaji wa Indonesia (Basarnas), Mohammad Syafii, amesema shughuli za uokoaji zimeongezwa, huku waokoaji wakitumia meli, ndege na vikosi maalumu vya uokoaji chini ya maji.
“Bado tuna matumaini ya kupata manusura zaidi,” alisema Syafii katika mkutano wa taarifa kuhusu operesheni hiyo.
Shirika la Habari la Marekani (AP) limeripoti kuwa takribani waokoaji 655 kutoka jeshi, polisi na taasisi nyingine wamehusishwa katika operesheni hiyo, huku meli na ndege 17 zikitumika kuwatafuta waliopotea.
Timu maalumu za wapiga mbizi pamoja na ndege zisizo na rubani zinazoweza kutumika chini ya maji pia zimeandaliwa kusaidia katika utafutaji.
Hata hivyo, hali ya bahari imekuwa kikwazo kikubw katika operesheni hiyo. AP imeripoti kuwa mawimbi yalifikia urefu wa takribani mita tatu wakati ajali ikitokea, huku upepo mkali ukiendelea kufanya iwe vigumu kwa waokoaji kufika karibu na meli hiyo.
Wizara ya Uchukuzi ya Indonesia imesema hadi leo Jumatatu, Septemba 14, watu 108 walikuwa wameokolewa, huku juhudi za kuwatafuta wengine zikiendelea.
Waziri wa Uchukuzi, Dudy Purwagandhi, amezielekeza taasisi zinazohusika kuweka kipaumbele katika utafutaji, uokoaji na utambuzi wa abiria waliokuwa ndani ya meli hiyo.
Kwa mujibu wa ABC News, Purwagandhi alisema mamlaka bado haziwezi kubaini iwapo baadhi ya waliopotea wako ndani ya meli hiyo au walichukuliwa na maji hadi maeneo mengine.
Amesema chanzo cha ajali bado kinachunguzwa ili kubaini iwapo ilisababishwa na hali ya hewa, hitilafu ya kiufundi au sababu za kibinadamu.
Shirika la habari la Indonesia, Antara, limeripoti kuwa vikosi maalumu vya Jeshi la Wanamaji vimejiandaa kushiriki katika utafutaji wa chini ya maji.
Meli ya kijeshi KRI Canopus, yenye vifaa vya kusaidia utafutaji chini ya maji, pia imewekwa tayari kwa operesheni hiyo.
Taarifa zinaeleza kuwa meli hiyo yenye urefu wa takribani mita 119 ilijengwa nchini Japan mwaka 1987 na ilikuwa imebeba pia magari 89.
Indonesia, yenye zaidi ya visiwa 17,000, hutegemea sana usafiri wa majini kama njia muhimu ya kusafiri kati ya visiwa.
Ajali hiyo imeongeza wasiwasi kuhusu usalama wa usafiri wa majini nchini humo, ambako ajali za vivuko zimekuwa zikitokea mara kwa mara.
Hadi jana, shughuli za utafutaji na uokoaji zilikuwa zinaendelea huku mamlaka zikisema hali ya hewa na mawimbi makubwa vinaendelea kuwa changamoto kwa timu zinazowatafuta watu waliopotea.
Habari hii imeandaliwa na Salma Hamisi kwa msaada wa mashirika ya habari ya kimataifa.

Back to Home
Sita wafariki dunia ajali ya meli, 129 hawajulikani walipo
Mwananchi about 3 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
