TRENDING
Tanapa inavyokuwa mfano wa usawa wa jinsia kwa taasisi za umma
Back to Home

Tanapa inavyokuwa mfano wa usawa wa jinsia kwa taasisi za umma

Mwananchi about 2 hours 3 mins read
Arusha. Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (Tanapa) limeongeza idadi ya wanawake katika nafasi za juu za uongozi hadi kufikia asilimia 37, kiwango kinachozidi wastani wa dunia wa chini ya asilimia 28 ya jinsi hiyo katika ngazi za maamuzi. Hatua hiyo, inaifanya Tanapa kuwa miongoni mwa taasisi za umma nchini zinazoongoza katika kuendeleza usawa wa kijinsia. Akizungumza jana Juni 23, 2026, Kamishna wa Uhifadhi wa Tanapa, Musa Kuji, amesema ongezeko hilo limetokana na juhudi za makusudi za shirika kupanua ushiriki wa wanawake kwenye nafasi za maamuzi na uongozi. “Uwakilishi wa wanawake katika nafasi za uongozi umeongezeka kutoka asilimia 22.6 mwaka 2020/2021 hadi asilimia 37 mwaka 2025/2026,” amesema. Kwa mujibu wa shirika hilo, wanawake sasa wanashikilia nafasi 23 kati ya nafasi 62 za ngazi ya ukamishna ndani ya Tanapa, hatua inayodhihirisha mabadiliko katika taasisi ambayo kwa miaka mingi iliongozwa zaidi na wanaume. Miongoni mwa wanawake wanaoshikilia nafasi za juu za uongozi ni Kamishna Msaidizi wa Uhifadhi, Moreen Mwaimale anayesimamia Fedha, Cecilia Mtanga anayesimamia Rasilimali Watu, Catherine Mbena anayesimamia Mawasiliano ya Shirika, Jully Lyimo anayesimamia Maendeleo ya Biashara, Catherine Mwamasage anayesimamia Manunuzi na Sekela Mwangota anayesimamia Mipango, Ufuatiliaji na Tathmini. Mbali na nafasi hizo za kimkakati, amesema wanawake pia wameendelea kupewa majukumu makubwa ya kiuendeshaji ndani ya shirika hilo. Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Uhifadhi, Dk Beatrice Kessy, anaongoza Kanda ya Kaskazini, moja ya kanda nne za kiutawala za Tanapa. Katika Ofisi za Kiunganishi za shirika hilo, wanawake pia wamepewa dhamana ya kuongoza maeneo muhimu ambapo Neema Mollel anaongoza ofisi ya Dar es Salaam, Dk Halima Kiwango anaongoza ofisi ya Zanzibar na Noelia Myonga anaongoza ofisi ya Dodoma. Katika ngazi ya usimamizi wa hifadhi za taifa, wanawake wanaongoza hifadhi nane kati ya 21 zinazomilikiwa na kusimamiwa na Tanapa. Miongoni mwao ni Angela Nyaki anayesimamia Hifadhi ya Taifa Kilimanjaro, Dk Tutindaga George wa Hifadhi ya Taifa Tarangire, Dk Yustina Kiwango wa Hifadhi ya Taifa Ziwa Manyara na Eva Mallya wa Hifadhi ya Taifa Mkomazi. Wengine ni Witness Shoo wa Hifadhi ya Taifa Arusha, Gladys Ng’umbi wa Hifadhi ya Taifa Saadani, Theodora Batiho wa Hifadhi ya Taifa Milima ya Udzungwa pamoja na Upendo Massawe anayesimamia Hifadhi ya Taifa Kisiwa cha Saanane. Ongezeko la uwakilishi wa wanawake katika nafasi za juu za uongozi limekuja wakati dunia ikiendelea kuhimiza ushiriki wa wanawake katika ngazi za maamuzi. Shirika la Umoja wa Mataifa la Usawa wa Kijinsia na Uwezeshaji wa Wanawake (UN Women) na Umoja wa Mabunge (IPU) zinaonyesha wanawake wanashikilia chini ya asilimia 28 ya nafasi za juu za maamuzi duniani. Kwa mujibu wa Tanapa, mafanikio hayo ya usawa wa kijinsia yamekwenda sambamba na kuongezeka kwa ufanisi wa utendaji wa shirika. Kuji, amesema kiwango cha ufanisi wa shughuli za Tanapa kimeongezeka kutoka asilimia 65 mwaka wa fedha 2020/2021 hadi asilimia 87 mwaka 2025/2026. “Matokeo haya yanatokana na uongozi shirikishi, mifumo imara ya uwajibikaji, ufuatiliaji wa karibu wa utendaji kazi na kuzingatia kwa upana masuala ya kijamii katika usimamizi wa taasisi,” amesema. Kwa upande wa Tanzania, hatua iliyofikiwa na Tanapa inaendana na juhudi za Serikali kukuza usawa wa kijinsia na kutekeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa (SDGs), yanayohimiza ushiriki sawa wa wanawake katika maisha ya umma na nafasi za maamuzi.

This article was sourced from an external publication.

Share this article

Comments (0)

Want to join the discussion?

Sign in to post comments and engage with the community.

Be the first to comment!

Airforce

View All

Armed Forces

View All
AD
OneClick Africa Logo

Africa's premier digital hub for impactful news, entertainment, and business insights.

© 2026 OneClick Africa. All rights reserved.