Shinyanga/Tanga/Tabora. Kuongezeka kwa matumizi ya pikipiki na bajaji, mahitaji ya abiria ya usafiri wa haraka, kukua kwa miji na mabadiliko ya maisha ni miongoni mwa sababu zinazotajwa kuchangia kupungua kwa usafiri wa abiria kwa baiskeli katika mikoa ya Tanga, Shinyanga na Tabora.
Kwa miaka ya nyuma, miji hiyo ilikuwa na utambulisho wa kipekee uliotokana na wingi wa baiskeli zilizotumika kusafirisha abiria na mizigo.
Baiskeli zilikuwa chanzo muhimu cha ajira kwa vijana na watu wenye mitaji midogo, huku baadhi ya familia zikitumia shughuli hiyo kugharamia mahitaji ya kila siku.
Hata hivyo, hali imebadilika. Pikipiki maarufu kama bodaboda na bajaji zimechukua nafasi kubwa katika usafiri wa mijini, zikivutia abiria kutokana na kasi, uwezo wa kufika maeneo mbalimbali na urahisi wa kusafiri kwa umbali mrefu ndani ya muda mfupi.
Mabadiliko hayo yameathiri si waendesha baiskeli pekee, bali pia mafundi, wauzaji wa baiskeli na wamiliki wa vituo vya usafiri huo.
Pikipiki zapunguza soko la baiskeli
Jijini Tanga, waendesha baiskeli wanaeleza kuwa biashara hiyo imepungua kwa kiasi kikubwa kutokana na kuongezeka kwa pikipiki.
Athuman Idd, ambaye amekuwa akiendesha baiskeli kwa zaidi ya miaka 20, anasema zamani kulikuwa na waendesha baiskeli wengi na wateja wa kutosha, hali iliyowawezesha kupata kipato kizuri.
Anasema moja ya faida kubwa ya biashara hiyo ilikuwa kutohitaji mafuta, kwa kuwa mwendeshaji alitumia nguvu zake mwenyewe kuendesha chombo hicho.
“Biashara ilikuwa na faida kwa sababu haikuhitaji mafuta. Ukiwa na nguvu na baiskeli unaweza kusafirisha abiria na mizigo na kupata fedha za kuendesha maisha,” anasema.
Hata hivyo, anasema ujio wa pikipiki umebadilisha tabia za abiria, wengi wakipendelea usafiri unaowawezesha kufika wanakokwenda kwa haraka.
Tofauti na kizazi cha zamani, kizazi cha sasa kinaonekana kuvutiwa zaidi na pikipiki kutokana na kasi na uwezo wake wa kumfikisha abiria kwa muda mfupi.
Salimu Kinega, mwenye umri wa miaka 22, ambaye ni mmoja wa waendesha bodaboda jijini Tanga, alisema mabadiliko hayo yanaonekana wazi kwa abiria wa sasa.
“Watu wengi ambao zamani walikuwa wakitumia baiskeli sasa wamehamia kwenye pikipiki kwa sababu wanataka usafiri wa haraka na unaoweza kuwafikisha maeneo mbalimbali kwa muda mfupi,” alisema Kinega.
Kwa upande wake, Muhina Omari, mtumiaji wa usafiri wa baiskeli jijini Tanga, anasema bado anaupendelea kwa sababu ya gharama yake kuwa nafuu, lakini anakiri kuwa pikipiki zimekuwa chaguo la watu wengi.
Vituo vya baiskeli vyapotea
Kupungua kwa abiria pia kumesababisha baadhi ya vituo vya baiskeli, maarufu kama vijiwe, kupoteza wateja au kufungwa.
Fundi wa baiskeli jijini Tanga, Mustakimu Mussa, ambaye amekuwa katika shughuli hiyo kwa zaidi ya miaka 20, anasema athari hizo zinaonekana pia kwenye sekta ya ufundi.
Anasema zamani alikuwa akitengeneza zaidi ya baiskeli 15 kwa siku, lakini kwa sasa idadi hiyo imeshuka hadi karibu nne.
“Vijiwe vimekufa. Zamani ukifika Barabara ya Kumi hukosi vijiwe vinne au vitano. Ukifika Kumi na Tatu ulikuta vitatu au vinne, vilevile Ngamiani kulikuwa na vijiwe sita au saba. Lakini sasa vimeuliwa na pikipiki,” anasema.
Kwa mujibu wa Mustakimu, hali hiyo imebadilisha pia aina ya biashara za watu waliokuwa wakitegemea baiskeli kama chanzo kikuu cha kipato.
Shinyanga, historia ya baiskeli yapungua
Shinyanga nayo imeshuhudia mabadiliko kama hayo. Kwa miaka ya nyuma, baiskeli zilikuwa sehemu muhimu ya maisha ya wakazi wa mji huo, zikifanya kazi kama chombo cha usafiri na wakati huo huo kuwa chanzo cha ajira.
Stephano Evarist, mwenye umri wa miaka 47, ambaye alianza kuendesha baiskeli za usafirishaji katika miaka ya 1990, anakumbuka kipindi ambacho familia nyingi zilimiliki baiskeli na kuzitumia kusafiri kutokana na uhaba wa usafiri wa magari.
Anasema wakati huo watu walikuwa tayari kusafiri umbali mrefu kwa baiskeli, tofauti na ilivyo sasa ambapo pikipiki na magari vimeenea.
“Miaka hiyo ya 1990 nilianza kuendesha baiskeli. Familia nyingi zilikuwa na baiskeli na tulisafiri masafa marefu. Wakati huo Simiyu ilikuwa bado wilaya, tulisafiri kutoka Shinyanga hadi Simiyu na hata Tabora kwa baiskeli,” anasema.
Kwa mujibu wa Stephano, maendeleo ya miji ya Kanda ya Ziwa yameambatana na kuongezeka kwa pikipiki na magari, hivyo kupunguza nafasi ya baiskeli katika usafiri wa abiria.
“Kwa sasa kumekuwa na maendeleo, usafiri wa baiskeli umepungua kwa kiasi kikubwa. Baadhi ya waendesha baiskeli wamebaki pembezoni, lakini katikati ya mji pikipiki ndizo zimejaa,” anasema.
Baiskeli ilikuwa mtaji kwa wenye kipato kidogo
Maganga Shija, dereva wa baiskeli za abiria kwa miaka 19, anasema kazi hiyo iliwahi kuwa fursa muhimu kwa watu wasio na ajira rasmi.
Alianza shughuli hiyo mwaka 2007 baada ya kupata mtoto wake wa kwanza, akitafuta chanzo cha ziada cha kipato.
Anasema kazi hiyo ilimsaidia kuhudumia familia yake ya watoto watano na pia kugharamia shughuli za kilimo.
“Nilipopata mtoto wa kwanza ndiyo niliamua kuingia rasmi kwenye hii kazi. Niliona nitafute kitu ambacho kitaniingizia kipato cha ziada,” anasema.
Anasema hali ya sasa ni tofauti kutokana na ushindani kutoka kwa pikipiki na bajaji.
“Kwa sasa ushindani umekuwa mkubwa sana. Angalau pale mafuta yanapopanda bei nauli huleta ahueni kwetu, lakini hali imekuwa mbaya. Tumebaki na wateja tuliowazoea,” anasema.
Tabora nayo yakumbwa na mabadiliko
Tabora, ambayo kwa muda mrefu ilikuwa miongoni mwa miji iliyotambulika kwa matumizi makubwa ya baiskeli, nayo imeathiriwa na mabadiliko ya mfumo wa usafiri.
Kuenea kwa pikipiki, bajaji na magari kumeifanya baiskeli kupoteza nafasi iliyokuwa nayo katika kusafirisha abiria. Ingawa bado baadhi ya wakazi hutumia baiskeli kutokana na gharama yake nafuu, usafiri huo hauonekani tena kwa wingi kama ilivyokuwa zamani.
Mabadiliko hayo yanaelezwa kuwa sehemu ya ukuaji wa miji na ongezeko la mahitaji ya wananchi ya usafiri wenye kasi na uwezo wa kuwafikisha mbali kwa muda mfupi.
Wito wa kuhifadhi historia
Pamoja na kupungua kwa matumizi ya baiskeli, baadhi ya wananchi wanaamini historia yake haipaswi kupotea.
John Mwendapole, dereva wa baiskeli mwenye umri wa miaka 27, anashauri historia ya baiskeli kama njia muhimu ya usafiri ihifadhiwe kupitia makumbusho, maonyesho na shughuli za kitamaduni, hasa katika miji ya Kanda ya Ziwa.
“Kuhifadhiwa kupitia makumbusho, maonyesho au shughuli za kitamaduni kunaweza kusaidia kizazi cha sasa kufahamu namna jamii ilivyotumia usafiri huo kabla ya kuenea kwa pikipiki na magari,” anasema.
Anashauri pia Serikali kuwaangalia waendesha baiskeli kama sehemu ya uchumi wa usafirishaji kwa kuwapatia mafunzo ya shughuli mbadala zinazohusiana na baiskeli.
Baiskeli inaweza kuwa fursa ya utalii
Mchambuzi wa uchumi na biashara, Nicodemus Mussa, anasema baiskeli ilikuwa mfano wa namna mtu mwenye mtaji mdogo alivyoweza kujiajiri katika sekta ya usafirishaji.
Anasema ujio wa pikipiki na bajaji haupaswi kutazamwa kama jambo baya, kwa kuwa ni sehemu ya maendeleo ya miji na mwitikio wa mahitaji ya wananchi ya usafiri wa haraka.
Hata hivyo, anasema historia ya miji iliyokuwa maarufu kwa baiskeli inaweza kugeuzwa kuwa fursa ya utalii na utamaduni.
“Baiskeli inaweza kuwa sehemu ya utambulisho wa miji iliyokuwa ikitumika. Tunaweza kuwa na njia maalumu za waendesha baiskeli, ziara za baiskeli na shughuli zinazowawezesha wageni kufahamu historia ya mji kupitia usafiri huo,” anasema.
Imeandikwa na Aurea Simtowe, Hellen Mdinda (Shinyanga) na Mbonea Herman (Tanga),

Back to Home
Usafiri wa baiskeli za abiria wazidi kupoteza umaarufu Tanga, Shinyanga na Tabora
Mwananchi about 2 hours 6 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
