Dar/mikoani. Matukio mawili ya ajali yaliyoripotiwa kutokea ndani ya siku nne yamepoteza uhai wa watu 14, huku ikiwajeruhi wengine 71 katika maeneo mbalimbali nchini.
Idadi hiyo ya vifo vya ajali ni sawa na wastani wa karibu watu wanne kila siku.
Hata hivyo, idadi hiyo haihusishi matukio ambayo hayajaripotiwa.
Ajali hizo, zimetokea kati ya Julai 30 na Agosti 2, mwaka huu, huku zote zikitokana na magari kugongana, katika Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma na nyingine Monduli, Arusha.
Matukio hayo ndio yaliyopoteza uhai wa wengi zaidi kwa wakati mmoja, ukilinganisha na ajali nyingine mbalimbali zilizotokea ndani ya mwaka huu.
Ajali iliyoua wanane
Katika Wilaya ya Bahi mkoani Dodoma jana, watu wanane walifariki dunia na wengine 66 kujeruhiwa kutokana na ajali iliyohusisha mabasi mawili yaliyogongana.
Ajali hiyo ilihusisha basi la Kampuni ya Isamilo, lililokuwa likitokea Mwanza kuelekea Dar es Salaam na Basi la Libanika Luxury, lililokuwa likitoka Dar es Salaam kuelekea Mwanza.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gallus Hyera alithibitisha kutokea kwa ajali hiyo.
"Ni kweli kuna ajali imetokea katika Wilaya ya Bahi ikihusisha mabasi mawili ya abiria, chanzo na nini limetokea, nitawajulishe kupitia taarifa kwa umma, naomba uvute subira," alisema alipozungumza na Mwananchi.
Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Rosemary Senyamule alithibitisha vifo vya watu wanane, akisema kati yao wanaume ni watano na wanawake watatu.
"Kwa masikitiko tumepoteza wenzetu katika ajali hiyo, watu saba walifariki papo hapo lakini mmoja amepoteza maisha wakati akiendelea kupatiwa matibabu katika hospitali ya rufaa ya mkoa," amesema Senyamule.
Amesema mabasi hayo yaligongana alfajiri katika Kijiji cha Ibihwa Wilaya ya Bahi, baada ya mmoja wa madereva alipokuwa akijaribu kulipita gari lililokuwa mbele yake bila kuchukua tafadhari.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma, Dk Ernest Ibenzi amekiri kuwapokea majeruhi 66 na kwamba wanaendelea na huduma katika hatua tofauti tofauti.
"Tumewapokea majeruhi 66, wengine wanatibiwa kwenye wodi za kawaida za majeruhi lakini baadhi wamepelekwa katika vyumba vya upasuaji na bado wanaendelea na kupatiwa huduma," amesema Dk Ibenzi.
Ajali iliyoua sita
Katika hatua nyingine, Julai 30, mwaka huu, watu sita walipoteza maisha kutokana na ajali iliyohusisha basi lililogongana na lori wilayani Monduli mkoani Arusha.
Ajali hiyo ilitokea saa 12:40 jioni katika barabara ya Arusha-Dodoma, Makuyuni wilayani Monduli, Mkoa wa Arusha.
Mbali na idadi hiyo ya waliopoteza maisha katika ajali hiyo, watu watano walijeruhiwa na kati yao wawili wameruhusiwa, huku watatu wakiendelea na matibabu.
Akizungumzia hilo jana, Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mount Meru, Dk Kipapi Mlambo amesema hadi Ijumaa mchana kulikuwa na majeruhi watatu wanaoendelea na matibabu.
Amesema wawili waliokuwa na majeraha yasiyo makubwa waliruhusiwa baada ya madaktari kuridhika na hali zao.
Ameeleza majeruhi hao wanaoendelea na matibabu, mmoja amevunjika mfupa wa shingo na baada ya kufanyiwa tathmini za kitabibu ameridhia kufanyiwa upasuaji.
“Kwa huyu mfupa wa shingo umevunjika,kuna njia mbili za matibabu, kufunga ili upone wenyewe au kufanya upasuaji. Ameomba kufanyiwa upasuaji na taratibu zimekamilika, atafanyiwa kesho,” amesema Dk Mlambo.
Amesema majeruhi mwingine alikuwa na majeraha ya kichwa pamoja na tatizo katika jicho, lakini anaendelea vizuri na ndugu zake tayari wamepatikana.
“Tumemshauri akae hapa kwa sababu jicho lake halijakaa vizuri kidogo,tunataka kuona maendeleo yake kabla ya kuamua hatua nyingine,” amesema.
Amesema majeruhi mmoja alipata majeraha zaidi katika taya na ulimi na amepewa rufaa kwenda Hospitali ya KCMC kutokana na kuhitaji huduma ya daktari bingwa wa taya.
Ameeleza kuwa, hali ya majeruhi huyo haikuruhusu kusafirishwa kwa sababu alikuwa akipata changamoto ya kupumua, lakini baada ya kuimarika ameandaliwa kupelekwa KCMC.
"Huyu wa tatu ndiye aliumia zaidi kuliko wengine, tunampa rufaa aende KCMC kwani kwa ubingwa tulionao hapa hautoshelezi kumtibu,ameshakaa vizuri leo na anaandaliwa leo apelekwe KCMC," alisema.
Ajali hiyo ilitokea usiku wa Julai 30, 2026 baada ya basi la Kampuni ya Kandahari, kugongana uso kwa uso na lori.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Justine Masejo, amesema watu sita walifariki dunia kutokana na ajali hiyo kati ya hao, watano walifariki papo hapo na mmoja alifariki wakati akipatiwa matibabu hospitalini.
Amesema waliofariki ni wanaume watatu na wanawake watatu.
Ajali hiyo, amesema ilihusisha basi hilo lililokuwa likitoka mkoani Kilimanjaro kuelekea Mpanda mkoani Katavi na lori lililokuwa likitoka Kahama mkoani Shinyanga kuelekea Tanga.
Amesema polisi wanaendelea na uchunguzi kubaini chanzo cha ajali hiyo, huku miili ya marehemu ikiwa imehifadhiwa katika Kituo cha Afya Makuyuni kwa ajili ya uchunguzi wa kitabibu na taratibu za utambuzi.
Katika tukio hilo, lori jingine lililokuwa nyuma ya lori lililogongana na basi lilipinduka baada ya dereva wake kujaribu kukwepa ajali hiyo.
Masejo, alitoa onyo kwa madereva wanaokiuka sheria za usalama barabarani, akisema vitendo kama kupita magari bila tahadhari katika maeneo yaliyokatazwa vinaweza kusababisha madhara makubwa.
“Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha linatoa onyo kwa baadhi ya madereva wasiozingatia sheria za usalama barabarani, ikiwamo kupita magari mengine bila tahadhari au sehemu ambazo alama na michoro ya barabara imekataza kufanya hivyo,” amesema.
Baada ya ajali hiyo, Jeshi la Polisi, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji pamoja na wananchi walifika eneo la tukio kusaidia kuwaokoa majeruhi waliokuwa wamenasa ndani ya magari na kutoa miili ya marehemu kwa ajili ya kutambuliwa na ndugu zao.
Imeandikwa na Janeth Mushi, Habel Chidawali na Filbert Rweyemamu

Back to Home
Ajali zilivyopoka uhai wa watu 14 ndani ya siku nne
Mwananchi 1 day 5 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
