Arusha. Mkurugenzi wa Bodi ya Maji Bonde la Pangani, Mhandisi Segule Segule amesema ushirikiano kati ya bodi hiyo na Jumuiya za Watumiaji Maji zimesaidia kulinda vyanzo vya maji, hatua inayoongeza uhakika wa upatikanaji wa maji katika maeneo mengi yanayosimamiwa na bonde hilo.
Hayo ameyasema leo Jumamosi, Agosti 8, 2026 kwenye maonyesho ya Nanenane Kanda ya Kaskazini juu ya usalama na uendelevu wa vyanzo vya maji kwenye Bonde la Pangani kuwa elimu ambayo wamekua wakiitoa kwa jamii na umuhimu wa maji katika matumizi ya kila imesaidia kulinda vuanzo hivyo.
Amesema Bonde la Pangani ni kati ya mabonde tisa ya maji nchini yakiwa na majukumu ya kusimamia rasimali maji kwaajili ya kusambaza maji kwaajili ya matumizi ya majumbani kupitia mamlaka za maji maeneo ya miji na vijijini huduma inatolewa na Wakala wa Maji na Usafi wa Mazingira vijijini (Ruwasa).
“Bodi za mabonde zimewekwa kuratibu matumizi ya hayo maji, kuyasimamia hayo maji kama rasilimali kwenye dhana yake ya rasilimali, sisi bodi za mabonde yote tunafanya kazi hiyo na kazi imeanza kufanyika tangu enzi ya mkoloni alikua pia watu kuchukua vibali maalumu kwa ajili ya matumizi ya maji,” amesema Segule.
Segule ameongeza kuwa sheria ya mwanzo ilitungwa mwaka 1974, ikieleza utaratibu wa usimamizi wa maji na mwaka 2009 zilitungwa sheria mbili, sheria inayohusika na usimamizi wa rasilimali za maji na sheria ya usambazaji maji na kutokea marekebisho mengine ya sheria za maji.
“Yeyote anayetaka kuchukua maji kutoka kwenye chanzo kikuu cha maji ni lazima apate kibali kwetu, kwetu chanzo ni chemchem, ukiona huo ni mto unatembea, ukiona hilo ni ziwa, ni bwawa hata kama umejenga bwawa lako, yale maji sio yako ila ile miundombinu ndiyo yako, lazima uje kuomba kibali tujue unahifadhi maji kiasi gani,” amesema Segule.
Kuhusu mabwawa, amesema sheria inataka Bodi hiyo ijue kabla ya kuchimba ili itoe kibali, ameongeza kuwa utaratibu wa watendaji kazi wa bodi unazingatia matumizi mapana ya maji kwa watumiaji kunufaika bila kuathiriwa na watumiaji wengine.
Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa ushiriki wao katika maonyesho hayo unalenga kuendelea kutoa elimu kwa wananchi ili watoe ushirikiano pale wanapoona wanaokiuka sheria taarifa zinatolewa kwa wakati ili vyanzo vya maji viwe endelevu kwa kizazi cha sasa na kijacho.
Ameongeza kuwa kutokana na umuhimu wa huduma ya maji kwa jamii na elimu ambayo imekuwa ikitolewa, matukio ya ukiukwaji wa sheria dhidi ya mabonde ya maji yamepungua kwasababu huduma ya maji haina mbadala katika matumizi ya kila siku majumbani.
Baadhi ya wananchi wanaoshiriki maonyesho hayo, Hilda Jacob amesema kushiriki kwake kumemwezesha kupata elimu juu ya utendaji kazi wa Bonde la Pangani katika usimamizi wa rasilimali maji.
“Sikua naelewa kama kuna taasisi nyingine inayosimamia huduma za maji zaidi ya Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Arusha (Auwsa), hii elimu inafaa iwafikie wananchi wengi hasa kulinda vyanzo vya maji kwasababu mgao wa maji kwa sisi tunaoishi maeneo ya nje kidogo na mji hatupati maji kulingana na mahitaji,”amesema Hilda
Maonyesho ya Nanenane Kanda ya Kaskazini yanayoendelea yamewaleta pamoja wakulima,wafugaji,taasisi za umma na binafsi wakiwemo wajasiriamali na wananchi kwa ujumla kujifunza mbinu mbalimbali za kuongeza tija kwenye shughuli zao.

Back to Home
Elimu ya utunzaji vyanzo vya maji imesaidia uhakika wa upatikanaji maji
Mwananchi about 2 hours 3 mins read
This article was sourced from an external publication.
Share this article
