TRENDING
Watatu wafariki dunia, wengine 48 kuokolewa ajali ya boti Ziwa Victoria
Back to Home

Watatu wafariki dunia, wengine 48 kuokolewa ajali ya boti Ziwa Victoria

Mwananchi about 2 hours 3 mins read
Mwanza. Watu watatu wamefariki dunia na wengine 48 wameokolewa baada ya boti iliyokuwa imebeba zaidi ya abiria 50 kuteketea kwa moto katika Ziwa Victoria usiku wa kuamkia leo Alhamisi, Julai 9, 2026. Waliofariki ni watu wazima wawili na mtoto mmoja mwenye umri wa miaka 10, huku manusura wakinusurika baada ya juhudi za uokoaji zilizofanywa na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kushirikiana na wavuvi wa eneo husika. Kaimu Kamanda wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Mkoa wa Mwanza, Elisa Mugisha, amesema katika taarifa iliyotolewa leo Alhamisi Julai 9,2026 kuwa operesheni ya uokoaji ilifanikiwa kuwaokoa watu 48. "Waliofariki ni watu wazima wawili wanaokadiriwa kuwa na umri wa miaka 70, mwanaume, na miaka 45, mwanamke, ambao utambulisho wao bado haujafahamika, pamoja na mtoto Godson Stephen mwenye umri wa miaka 10," amesema Mugisha. Amesema boti hiyo inayomilikiwa na Paschal Ng'hwang'hwa, iliteketea kabisa pamoja na mizigo iliyokuwa ndani yenye uzito unaokadiriwa kufikia tani 6.5. Mugisha amesema uchunguzi wa kubaini chanzo cha moto unaendelea na Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kwa kushirikiana na mamlaka nyingine husika. Aidha, ametoa pole kwa familia zilizopoteza ndugu na jamaa zao katika tukio hilo na kuwataka wananchi, wamiliki wa vyombo vya usafiri majini na wadau wa sekta hiyo kuendelea kuzingatia kanuni na taratibu za usalama ili kupunguza madhara yanayoweza kujitokeza wakati wa dharura. Kwa mujibu wa Kaimu Ofisa Mfawidhi wa Ofisi ya Shirika la Uwakala wa Meli Tanzania (Tasac) Mkoa wa Mwanza, Paul Msokwa, taarifa za tukio hilo zilipokewa saa 11:00 alfajiri, na mara moja vikosi vya uokoaji vikaanza operesheni iliyowezesha kuwaokoa watu 48. Amesema katika awamu ya kwanza waliokolewa watu 33 na kupelekwa Bwiro, huku watu wengine 15 wakiokolewa baadaye na kupelekwa Kisiwa cha Lyamwenge kilicho jirani na Kisiwa cha Kunene. "Watu waliookolewa katika awamu ya kwanza walipelekwa Hospitali ya Wilaya ya Nansio kwa ajili ya kupatiwa matibabu, huku waliobaki wakipelekwa eneo la Bwiro lililopo kati ya visiwa vya Kunene na Lyamwenge ambako tukio hilo lilitokea," amesema Msokwa. Akizungumzia usalama wa usafiri wa majini, Mwenyekiti wa Soko la Samaki la Kimataifa la Kirumba Mwaroni, Fikiri Makafu, ameiomba Serikali kufanya jitihada za kurejesha huduma ya meli ya MV Clarias, akisema ilikuwa msaada mkubwa kwa wakazi wa visiwa vya Ziwa Victoria. "Kuwepo kwa meli hiyo kulikuwa mkombozi mkubwa kwa wakazi wa visiwa. Ikiendelea kutoa huduma, kiwango cha usalama kitaongezeka kwa kiasi kikubwa," amesema. Baadhi ya manusura wamesema safari ilianza saa 3:00 usiku kutoka Kisiwa cha Gozba, lakini ilipofika saa 7:00 usiku boti hiyo ilikumbwa na moto uliosababisha taharuki kubwa. Emmanuel Aloyce, ambaye alikuwa baharia wa boti hiyo, amesema awali waligundua mfumo wa maji wa kupoza injini ulikuwa umeziba na baadaye moto ukazuka. "Baada ya kugundua moto umetokea, nilitumia mafunzo niliyopata kuwaelekeza abiria wote kuvaa maboya. Hatua hiyo ndiyo iliyochangia kwa kiasi kikubwa kuokoa maisha yetu," amesema. Naye manusura mwingine, Elia Samweli, amesema alikuwa amelala wakati tukio hilo lilipotokea na alishtuliwa na sauti ya mhandisi aliyekuwa akiwataka abiria waamke haraka. "Nilikuwa nimelala. Kilichonishtua ni sauti ya mhandisi akisema, 'Amkeni, tumekwisha.' Nilipoamka nilikuta moto umewaka kwenye boti. Sikujua chanzo chake, lakini nilichukua boya langu na kuruka majini kama walivyofanya wengine. Namshukuru Mungu nimepona," amesema. Boti hiyo ilikuwa ikisafirisha abiria pamoja na mizigo kutoka Kisiwa cha Gozba mkoani Kagera kuelekea Mwanza kabla ya kuteketea kwa moto katikati ya Ziwa Victoria.

This article was sourced from an external publication.

Share this article

Comments (0)

Want to join the discussion?

Sign in to post comments and engage with the community.

Be the first to comment!

DR Congo

View All

Somalia

View All
AD

Senegal

View All

Traditional Affairs

View All
AD
OneClick Africa Logo

Africa's premier digital hub for impactful news, entertainment, and business insights.

© 2026 OneClick Africa. All rights reserved.